Ads (728x90)

Powered by Blogger.




Na Seleman Juma- Songea

Katika mwambao wa ziwa Nyasa, mamba walikuwa tishio kwa wananchi wanaozunguka ziwa hilo kutokana na ukweli kwamba watu wengi walipoteza maisha kwa kuliwa ama kuuliwa na mamba pindi wanapoogelea au kuvua samaki.


Jambo la mamba kushambulia watu, lilihusishwa na Imani za kishirikina, wakati mwingine walikuwa wakitishiana kwamba ukinizingua nitakutumia mamba akuue. Kwa kweli mamba waliweka hofu kubwa miongoni mwa wanajamii.

Wataalamu wanasema kuna aina kumi na tano (15) za mamba. Inadaiwa kuwa mamba anaweza kuishi kati ya miaka sabini (70), mia moja na hamsini (150) na pengine hadi mia tatu (300).

Wataalamu wanasema kuwa, mamba ana urefu wa mita saba (7) na ana uzito wa zaidi ya kilo elfu moja 1000 na anakula mara moja kwa wiki kati ya kilo ishirini (20) hadi ishirini na tano (25). 

Sambamba na hilo, mamba akiwa majini ana nguvu sana hata kama mtu au mnyama akawa na kilo nyingi lakini anakuwa mwepesi anapokamatwa na mamba majini. Pengine watu wanaoishi karibu na maziwa kama vile; Vikitoria, Tanganyika, Rukwa, Nyasa bila shaka wanamjua Mamba kwa usahihi zaidi.

Habari hii ya mamba inanirudisha nyuma nikiwa nasoma pale Kantalamba Sekondari Sumbawanga mwaka 2007-2009 maana tulikuwa tukisimuliwa na wenyeji jinsi mamba wa Ziwa Rukwa walivyokuwa wakiua watu. Sasa nipo mkoani Ruvuma bado Habari ni ileile.

Lakini tatizo la mamba kuua watu mwambao wa Ziwa Nyasa lilikomeshwa na Mzee John Mpembo mstaafu wa Jeshi la Wananchi la Tanzania (JWTZ) ambaye ni marehemu kwa sasa. Mungu aiweke Roho yake mahali pema peponi amina!
Pamoja na kwamba mzee Mpembo hatunae tena Duniani, atakumbukwa zaidi kwa kazi ngumu, nzito na ya hatari ya kuua mamba katika Ziwa Nyasa ambao walikuwa tishio kwa wananchi wanaolizunguka Ziwa hilo.

Mzee Mpembo, maarufu kwa jina la ‘Mrema’ hawezi kusahaulika na wananchi wa mwambao wa Ziwa Nyasa mkoani Ruvuma baada ya kufanikiwa kukomesha tatizo la mamba kuua watu lililohusishwa na imani za kishirikiana ambalo lilikithiri hasa katika maeneo ya Liuli na Mbambabay.

Kwa mujibu wa taarifa ya Afisa Habari wa Manispaa ya Songea, Albano Midelo ambaye alifanya mahojiano na Mzee Mpembo kabla hajafari, inaonesha kuwa mnamo mwaka 1992, mzee Mpembo alianza jukumu la kupambana na mamba katika ziwa Nyasa.

Taarifa inaonesha kuwa, Mzee Mpembo alianza operesheni ya kuua mamba baada ya kupata kibali toka Wizara ya Maliasili na Utalii mwaka 1991 baada ya mauaji ya mamba kukithiri mno na kutishia usalama wa maisha ya watu wanaofanya shughuli zoa katika Ziwa Nyasa.

Mauaji ya Mamba kwa raia wawili (2) wa kigeni  ya mwaka 1991 yalimfanya mzee Mpembo kuomba kibali wizara ya Maliasili na Utalii ili kunusuru maisha ya watanzania pamoja na raia wa kigeni wanaozuru  Ziwa Nyasa kwa ajili ya utalii.
Baada ya kupata kibali, Mzee Mpembo alianza operesheni yake kwa kutumia ndoano maalum iliyowekwa nyama ya mbwa na alifanikiwa  kuwaua mamba 607 na kukomesha tatizo hilo.

Kwa sasa matukio ya mamba kuuwa watu yamepungua katika mwambao wa Ziwa Nyasa jambo ambalo litaongeza chachu ya utalii katika Ziwa Nyasa.

Kwa mjibu wa Wikipedia, Ziwa Nyasa ni kati ya maziwa makubwa ya Afrika ya Mashariki likiwa na nafasi ya tatu baada ya Ziwa Viktoria na Ziwa Tanganyika ya nchini Tanzania. Lina urefu wa km 560 na upana wa km 50-80. Vilindi vyake vinaelekea hadi mita 704 chini ya uwiano wa maji yake.

Ziwa Nyasa linapatikana kati ya nchi za Tanzania, Malawi, na Msumbiji. Kusini mwa Ziwa unatoka Mto Shire unaopeleka maji kwenye Mto Zambezi na hatimaye Bahari Hindi. Kijiolojia ziwa ni sehemu ya Bonde la Ufa la Afrika ya Mashariki.
Ziwa Nyasa linajulikana kuwa na aina nyingi za samaki (zaidi ya 1500). Aina chache tu zinavuliwa kama chakula, lakini aina mbalimbali zinakamatwa na kuuzwa nje ya Afrika kwa wapenzi wa samaki wa rangi.

Kwa mantiki hiyo, Ziwa Nyasa sasa ni sehemu nzuri ya utalii, hivyo watanzania hatuna budi kufanya utalii wa ndani kwa lengo la kukuza uchumi wa nchi yetu. Lakini pia, usalama uliopo katika Ziwa Nyasa ni chachu ya utalii kwa wageni wanaotoka nchi za nje.

Shughuli za kiuchumi katika mwambao wa Ziwa Nyasa kwa sasa zitakuwa kwa kasi zaidi baada ya kukamilika kwa uundaji wa meli mbili za mizigo maarufu kama ‘MV Ruvuma’ na ‘MV Njombe’ ambao umekamilika kwa asilimia 99% zitasaidia kuchochea uchumi wa nchi.

 Hivi karibuni tumeshuhudia Mkurugenzi wa Kampuni ya Songoro Marine Transport Bw. Salehe Songoro akiwa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Eng. Edwin Ngonyani wakikagua  ujenzi wa meli  hizo mbili za mizigo katika bandari ya Itungi Ziwa Nyasa.

Mantiki hiyo, wafanyabiashara wa Mbeya, Njombe, Iringa, Ruvuma na nchi jirani za Msumbiji na Malawi hawana budi kutumia Ziwa Nyasa katika usafirishaji wa bidhaa zao kutokana na uwepo MV Njombe na MV Ruvuma.

 Maoni ya wakazi wa Ruvuma

Maoni haya yalitolewa na wakazi wa Mkoa wa Ruvuma kwa njia ya Mtandao wa kijamii maarufu kama “Facebook”.

Rehema Mapunda anasema kuwa,  kweli imebaki Story, wakati akiwa shule hizo habari za mamba kula watu, zilikuwa zinatisha mno, na kila mtu aliyekuwa anatoka Nyasa (mnyasa) alimuona kuwa mchawi, aliamini kuwa ukimuudhi  Mnyasa anaweza kukutumia mamba.

“Kweli  Mzee Mpembo (Mrema) aliutumia vizuri ujuzi wake wa kijeshi kutatua tatizo la mamba kuua watu ziwa Nyasa, hongera sana mzee wetu na Mungu akulaze mahali pema peponi amina!”, alisema Mapunda.

Emanuel Liganga anasema kuwa huyo Mzee Mpembo anamkumbuka sana na alikuwa akishirikiana  naye kutafuta mbwa wa chambo kwa kunasia Mamba, tangu  miaka ya1990's. 

“Mzee huyu namkumbuka sana mimi, kumbukumbu yangu inaonesha kuwa mwanzoni mwa mwaka  2002  aliua mamba wawili pale Mbamba Bay baada ya kuuliwa rafiki yangu na mdogo wangu kipenzi Freddy Mponda. Lakini hiyo idadi ya mamba aliyoitaja ina ukakasi, sijaiamini, labda aliteleza kwenye kuitaja”, alisema Liganga.

Kwa upande wake, Nyimbi Ernest  alisema kuwa, Habari ya mzee John Mpembo inamkumbusha mbali sana maana kipindi cha nyuma Nyasa ilisifika kwa uchawi wa kutumia  Mamba kumbe ilikuwa ni Imani potofu tu. “Siwezi kumsahau mtu maarufu kama John John, hongera kwa kuweka kumbukumbu muhimu kama hii”, alisema.

Mariot Salimu alisema kuwa, alisikia habari za mzee Mrema na baadae alifanikiwa kumwona kwa macho yake mawili eneo la LUNDO akiua mbwa kwa ajili ya shughuli ya uwindaji wa mamba katika Ziwa Nyasa. 
(0759 388023)


Post a Comment