Ads (728x90)

Powered by Blogger.




Na Padri Titus Amigu


Vijana tunaendelea na mada zetu. Nadhani nimewapeni muda wa kutosha kutafakari mada yetu ya mwisho, yaani juu ya imani inayotudumaza ya “uchawi” au “ushirikina”.


Leo nina mada ya ajabu kidogo, lakini ndiyo itakayoweza kuweka wazi sababu ya malumbano yanayojitokeza au pengine yanayoendelea kati yetu Wakristo. Kifupi, mzizi mkuu wa malumbano yetu ni kuwapo kwa Biblia kubwa na Biblia ndogo na hivyo kuwa na Mungu mkubwa na mungu mdogo.


Wakristo tuna Biblia mbili na hivyo inaonekana tuna miungu miwili, Mungu mkubwa wa Biblia kubwa na mungu mdogo wa Biblia ndogo. Hiki ni kisa cha kushangaza, lakini ndivyo kilivyo, na leo nitasema ukweli ili mambo yawe bayana kwetu sote.


Hiki ni kisa cha Kanisa Katoliki kuwa na Biblia kubwa na hivyo kuwa na Mungu mkubwa kuliko mungu wa makanisa mengine.
Hebu nianze na jambo lililo dhahiri zaidi. Wala hatuna mashaka, tuna Biblia mbili tofauti, Biblia kubwa (vitabu 72 au 73) na Biblia ndogo (vitabu 66).


Kumbe, kwa vile makanisa mengine yana Biblia ndogo, yaani ya vitabu 66 tu, yana Mungu mdogo. Nahukumu kwa kufuata maweza yao. Yupo mungu mdogo kwa sababu hajui na wala hawezi mengi sana.


Mungu mdogo hatofautiani sana na mimi Pd. Titus Amigu. Atakuwa hajui mengi ya kesho. Atakuwa hakumbuki alichosema. Atakuwa mwongo. Ataweza kusingiziwa mengi na kadhalika. Mkasa huu unatokeaje? Unatokea kwa sababu Biblia ya vitabu 66 ni ndogo.



Udogo huu ni pendekezo la mwanadamu mmoja tu. Ni hivi, udogo huo umetokana na Martin Luther, hapo mwaka 1517 kuchagua kuwafuata Wayahudi wa Palestina ambao walivikataa vitabu vya Wayahudi wenzao waliokuwa wakikaa huko Aleksandria, Misri.


Wayahudi waliokuwa wakikaa nje ya Palestina (Diaspora) walikuwa na vitabu vingi zaidi. Inaonekana jamii yao ilikuwa na waandishi wengi hodari.


Jambo hilo si ajabu. Wamakonde, Wandonde, Waigbo, Wanubi, Wajerumani, Wamarekani au Wachina wanaokaa nje ya nchi yao wanaweza kuwa hodari zaidi kuliko watu waliobaki kwao.


Kumbe, Wayahudi waliokuwa wakikaa nje ya Palestina, ndio Diaspora, waliandika vitabu vingi vizuri. Ndiyo kisa walipovitafsiri vitabu hivyo katika Kigiriki wakatoka na vitabu vingi zaidi kuliko wenzao waliobaki Palestina.


Tafsiri hii ya Maandiko ilifanywa huko Misri chini ya ushauri wa Mfalme Philadelphus (Ptolemy II) katika miaka ya 285 -247 Kabla ya Kristo.


Kwa taarifa yako, Wakatoliki wanafuata orodha yenye vitabu 45 au 46 katika Agano la Kale na vitabu 27 katika Agano Jipya. Agano la Kale lina vitabu 45 au 46 kutokana na kusigana katika kuvihesabu vitabu viwili, kitabu cha Nabii Yeremia na kile cha Maombolezo. Baadhi ya watu huvihesabu kama vitabu viwili kutokana na kusadiki kwamba vimeandikwa na waandishi wawili tofauti wakati watu wengine husema vitabu hivyo vimeandikwa na mwandishi mmoja na hivyo ni kitabu kimoja tu. Kumbe, vitabu hivyo vikihesabiwa kama viwili, Agano la Kale linakuwa na vitabu 46 wakati vikihesabiwa kama kimoja , idadi ya vitabu vya Agano la Kale hushuka kwa kitabu kimoja na hivyo kuwa 45 tu.

Makanisa ya Kiprotestanti hufuata orodha iliyokuwa au inayofuatwa bado na Wayahudi huko Palestina, orodha yenye vitabu 24 katika Agano la Kale kutokana na kuvihesabu vitabu vyote 12 vya manabii wadogo (Hosea, Yoeli, Amosi, Obadia, Yona, Mika, Nahumu, Habakuki, Sefania, Hagai, Zekaria na Malaki) kama kitabu kimoja. Lakini, vitabu hivyo vikitenganishwa na kuhesabiwa kimoja kimoja, orodha hiyo hutanuka na idadi ya vitabu kupanda hadi 39 katika Agano la Kale.

Vitabu saba na sehemu za vitabu zinazoleta tofauti hiyo ni vitabu vya Tobiti, Yudithi, 1 na 2 Makabayo, Hekina ya Sulemani, Yoshua ben Sira, Baruku na Barua ya Yeremia pamoja na sehemu zifuatazo: Wimbo wa Vijana Watatu kwenye Tanuru (Dan 3:24-90), Simulizi la Susana (Dan 13) na Hadithi ya Bel na Joka (Dan 14).


WAYAHUDI WA DIASPORA WALIKUWA NA VITABU ZAIDI: Tunaulizana. Kwa nini Wayahudi wa Diaspora walikuwa na vitabu zaidi?


Asili ya tofauti hii ni ukweli kwamba hapo zamani kabla ya orodha ya vitabu (canon) vya Agano la Kale, yaani Biblia ya Kiyahudi haijafungwa rasmi, Wayahudi waliokuwa wakiishi uhamishoni, yaani nje ya Palestina (Diaspora), walikuwa na vitabu vingi zaidi kuliko vile walivyokuwa navyo Wayahudi wenzao waliokuwa wakiishi bado huko Palestina (Israeli au Uyahudi).


Nimeshaomba jambo hili lisichukuliwe kama ajabu ya pekee sana kwani uandishi waweza kustawi popote pale hata nje ya nchi fulani. Kwa hali hii, tunaweza kusema kwamba huko nje ya Palestina walikuwepo Wayahudi waandishi wazuri wengi zaidi.


Ukweli huu unashuhudiwa na taarifa iliyotufikia kwa kumbukumbu ya Barua ya Aristes. Barua hiyo inasimulia kwamba Wayahudi wa huko Aleksandria (Misri) walipoonekana wakishindwa kusoma vitabu vyao vya dini katika lugha ya Kiebrania, mfalme Philadelphus (Ptolemy II) aliyeishi kati ya 285 na 247 K.K. aliamua kuwasaidia kuvitafsiri vitabu vyao katika lugha ya Kigiriki kilichotawala katika Diaspora.


Basi, waliitwa watafsiri kutoka Israeli sita sita kutoka kila kabila la Israeli. Hivi, jumla yao kutoka makabila 12 ilikuwa 72 (au 70 kwa makumi ya karibu). Barua ya Aristes inasema watafsiri hao walifungiwa katika vyumba 72 tofauti kila mmoja na kutafsiri vitabu alivyopewa katika siku 72.


Barua inatangaza ajabu kubwa kwamba mwishoni mwa kazi yao, tafsiri zao zilipolinganishwa, zilifanana neno kwa neno. Kumbe, hii ndiyo tafsiri maarufu ya Agano la Kale inayojulikana kwa Kilatini hadi leo hii kama Septuaginta (yaani 70 ambayo kwa Kilatini huandikwa hivi LXX).


Lakini ajabu kubwa zaidi ilikuwa kwamba, kiidadi, vilipolinganishwa vitabu vya Agano la Kale la Septuaginta, ilizidi vile vilivyokuwa vikisomwa huko Palestina (Israeli au Uyahudi) kwa vitabu saba na sehemu za vitabu nilizotaja hapo juu.


JE, WAKRISTO WA MWANZO WALIPOKEA TAFSIRI YA SEPTUAGINTA? Ndiyo, tena ndiyo kubwa, kwani tangu enzi hizo, ndiyo karne ya kwanza na ya pili, Agano la Kale la tafsiri ya Septuaginta ndilo lililopokelewa na Kanisa la Kristo.


Hiyo ndiyo tafsiri iliyopokelewa na kutumika sana na mababa wa Kanisa, kama vile, Tertuliani, Ambrose, Augustino wa Hippo na kadhalika hasa kwa vile walikuwa weledi wa Kigiriki na hawakujua Kiebrania cha kutosha.


Zaidi ya hayo, tafsiri ya Septuaginta ambayo ilikuwa katika Kigiriki ilioana vyema na vitabu vya Agano Jipya (27) ambavyo tangu mwanzo viliandikwa katika Kigiriki cha kawaida (ndiyo koine, yaani Kigiriki cha kawaida) wakati vitabu vya Wayahudi huko Palestina vilikuwa bado vikitumiwa katika Kiebrania, tena Kiebrania cha zamani.


Basi, Agano la Kale la tafsiri ya Septuaginta likapata kuwa sehemu ya Biblia ya Kanisa la Mungu hata ikatafsiriwa pamoja na Agano Jipya katika Kilatini cha kawaida (ndiyo Vulgata) na akina Mt. Jerome, msimamizi wa taaluma ya Biblia.


Kumbe, ndiyo Biblia (LXX na Agano Jipya) hii iliyotumika na Kanisa na Wakristo wa Magharibi (kwani Wakristo wa Mashariki, ndio Waorthodoksi wana orodha ya vitabu vya Biblia kubwa zaidi, yaani vitabu zaidi ya 73) hadi karne ya 16. Septuaginta ilikuwa na vitabu 45 au 46 kujumlisha vitabu 27 vya Agano Jipya na hivyo kufanya Biblia ya Kanisa la Mungu kuwa na jumla ya vitabu 72 au 73.


Lakini, ajabu ya kupinduka chali ikatokea katika karne ya 16. Ni katika karne hii, Martin Luther aliposababisha mtengano wa Kanisa naye kuifumua Biblia kwa kuviondoa vitabu vile saba na sehemu za vitabu nilizowatajia, yaani, Tobiti, Yudithi, 1 na 2 Makabayo, Hekima ya Sulemani, Yoshua bin Sira, Baruku na Barua ya Yeremia pamoja na Wimbo wa Vijana Watatu kwenye Tanuru (Dan 3:24-90), Simulizi la Susana (Dan 13) na Hadithi ya Bel na Joka (Dan 14).


Ndiyo kusema basi, tangu wakati wa Martin Luther, Wakristo wote wanaojitenga na Kanisa Katoliki huamua kumsikiliza Martin Luther na hivyo kuiacha orodha ya Septuaginta (yaani Biblia ya Wayahudi wa uhamishoni) na kuifuata ile ya Palestina, yaani ile yenye vitabu pungufu kwa saba na ushehi. Ndiyo kisa basi, hadi leo hii, makanisa yote ya Kiprotestani na madhehebu yake mapya yanayozaliwa kila kukicha, hufuata orodha yenye vitabu vichache wakati Kanisa Katoliki likiendelea na orodha ile asilia kwa Wakristo yaani Septuaginta.


Hivi, kuhusu idadi ya vitabu kwenye Biblia, asikudanganye mtu yeyote yule, iwe amekujia na “suitcase” au na mkoba wa ngozi ya mbuzi.


Si kwamba WAKATOLIKI WAMEONGEZA VITABU kwenye Biblia isipokuwa ni kinyume chake kwani ukweli ni kwamba Martin Luther AMEVIPUNGUZA VITABU kwenye Biblia.


Usinikodolee macho! Unashangaa nini? Hii ni hesabu ya kawaida, hata chekechea haiwashindi kuilewa. Kama ukianza na namba 72 au 73 ukashuka hadi 66 maana yake umetoa au umepunguza.


Ingekuwa kwamba mtu ameanza na namba 66 na kupanda nayo hadi 72 au 73 ingekuwa kweli ameongeza. Kumbe, haikuwa hivyo, katika historia ya orodha rasmi ya vitabu vya Biblia, yaani canon.


Nadhani tumeelewana kabisa. Haya tuendelee. Hoja ya kufuata orodha ya vitabu vichache ni kwamba makanisa yaliyojitenga, kwa kadiri ya mawazo ya Martin Luther, huona kwamba vitabu vile vya ziada na sehemu zile za nyongeza havikuvuviwa, yaani havikuangaziwa na Roho Mtakatifu katika uandishi wake.


Ndipo, basi, Wakristo wote wanaomsadiki, kumsikiliza na kumfuata Martin Luther, huita vitabu hivyo na sehemu za Maandiko nilizozitaja kwa msamiati wa Kigiriki ‘apokrifa’.


Kumbe, Kanisa Katoliki, kwa upande wake, linavitambua bado vitabu hivyo pamoja na sehemu zile za nyongeza kwamba vimevuviwa na kwamba vinastahili kuitwa orodha ya nyongeza, ama kwa maneno mengine, ORODHA YA PILI ya vitabu vitakatifu, maana vimetoka kwa Wayahudi wenyewe tena wakati ule ule waandishi wengine wa kimungu walipokuwa wakiyaandika Maandiko Matakatifu katika nchi ya Palestina (Israeli au Uyahudi).


Ndipo basi, Kanisa katoliki huviita vitabu hivyo na sehemu nilizokutajia kwa jina lililotoholewa kutoka Kigiriki, ‘DEUTEROKANONI’, yaani ‘ORODHA YA PILI’.
MASWALI MADOGO MAWILI:


Swali 1. Pd Martin Luther alitoa hoja kuwa havikuvuviwa na Roho Mtakatifu. Lakini Kanisa Katoliki linatambua vilivuviwa na Roho Mtatikatifu kwa kuwa vilitoka kwa Wayahudi walewale japo walikuwa uhamishoni.


Je, wakati wa kukusanya vitabu vya Biblia Wayahudi waliwakataa Wayahudi wenzao waliokuwa uhamishoni walipokuja na mafundisho ya Biblia ile ile??


Jibu: Ndiyo, Wayahudi waliwakataa Wayahudi wenzao. Kiujumla, Wayahudi wa Palestina walivikataa vitabu tulivyovitaja pamoja na sehemu za vitabu ya Esta na Danieli. Walivikataa hasa kwa sababu Wakristo walikuwa wanavitumia tayari katika kufafanulia mafundisho yao.


Ndiyo kisa, kuvikataa huku kulifanyika huko Jamnia mwaka 95 Baada ya Kristo. Kabla yake, vitabu hivyo vilikuwa vinatumika kwa kujulikana kabisa, kwa mfano kitabu cha Yoshua ben Sira kilikuwa kikitumika na Wayahudi wote kama kitabu cha kiada katika kuwafundisha vijana maadili.


Swali 2. Je, Kanisa Katoliki limezingatia hoja zipi za msingi zinazosahihisha hoja alizotumia Pd. Martin Luther katika kuvipunguza vitabu hivyo ukiachana na hiyo ya kuvuviwa na Roho Mtakatifu alikosema.


Jibu: Hoja ya kwanza - kukataa kwa Martin Luther kunabainisha kwamba hakujua Maandiko Matakatifu maana nukuu za vitabu alivyovikataa zipo kwa namna moja au nyingine katika nukuu za waandishi wa vitabu vya Agano Jipya, kwa mfano, Waraka kwa Waebrania na nyaraka kwa watu wote zaYakobo na Petro.


Hii inamaanisha alikataa kitu ambacho kipo kwenye Biblia tayari. Ilikuwa kama mtu kukataa nyama iliyokaa juu ya wali wakati mchuzi wake umeshachanganywa na wali huo huo unaokula.


Hoja ya pili: Mafundisho ya vitabu alivyovikataa yalikuwa yanajulikana na jumuiya za Kikristo, yalikuwa hayapingani na mafundisho yaliyokuwa kwenye vitabu alivyovikubali, yalikuwa mafundisho yanayoweza kuhimiza imani na upendo na kadhalika, mambo ambayo kwa yenyewe yalikuwa vigezo (criteria) vya kuteulia vitabu vilivyoingia katika orodha ya vitabu vya Agano Jipya vilivyoandikwa na Wakristo wenyewe.


Huenda nimekuporomoshea mambo mapya mno na huenda, kichwani na moyoni mwako, unadhani nimesahau hoja ninayoijenga. La hasha! Nimekutaarifu kwamba Biblia ya Wakristo ilipunguzwa kutoka vitabu vya asilia 72 au 73 hadi vitabu 66.


Kwa mkasa huo, Biblia ilifanywa NDOGO na kwa kufanywa huko ndogo Mungu akakumbwa na balaa la kupunguzwa kutoka Mungu mkubwa hadi kuwa MUNGU mdogo.


Kwa nini? Kwa sababu mambo anayoshuhudiwa katika vitabu vile 7 na sehemu zilizokanwa na Martin Luther yatakanwa kwake. Sasa hivi nitakupa mifano kusudi usipupe pupe kana kwamba nimekunasisha kwenye mtego wa kware. Katika mada zote nakusudia kukuelimisha vyema.


MIFANO YA KUPUNGUZA VITABU SABA KULIVYOATHIRI MAFUNDISHO YA KIKRISTO


1. KWA KUKATAA KITABU CHA TOBITI, lazima mtu ukatae fundisho la watakatifu na malaika kuwa na uwezo wa kuwaombea wanadamu kwa maana jambo hilo limeshuhudiwa na Tobiti 12:11-21. Hapa pameandikwa hivi:


“‘Sasa nitawajulisheni ukweli wote bila kuwaficheni chochote. Nilikwishawaambia kwamba yafaa kuitunza siri ya mfalme, lakini matendo ya Mungu lazima yatangazwe kila mahali kama ipasavyo.


Tobiti! Wewe ma Sara mlipokuwa mnasali wakati ule, mimi ndiye niliwasilisha sala zenu mbele ya Bwana aliye mtukufu. Na kila ulipokuwa unawazika wafu, mimi niliwasilisha matendo yako mbele yake.


Wakati wewe hukusita hata kidogo kuinuka na kukiacha chakula ukaenda kumzika mtu aliyekufa, Mungu alinituma nikujaribu. Lakini pia alinituma kukuponya na kumwokoa mke wa mwanao, Sara. Mimi ni Rafaeli, mmoja wa wale malaika saba wanaokaa tayari daima mbele yake Bwana aliye mtukufu kumtumikia’.


“Tobiti na Tobia wakashikwa na hofu kubwa, wakasujudu wakiogopa sana. Lakini Rafaeli akawaambia: ‘Msiogope! Muwe na amani. Mtukuzeni Mungu milele.


Mimi nilipokuwa kati yenu haikuwa kwa kutaka kwangu mwenyewe, bali kwa kutaka kwake Mungu. Yeye ndiye mnayepaswa kumsifu.


Ninyi mlidhani mliniona nikila chakula, lakini ni kwa kuonekana tu na haikuwa hivyo. Basi, sasa mtukuzeni Bwana duniani na kumshukuru. Mimi narudi sasa kwake yeye aliyenituma kutoka juu.


Andikeni mambo hayo yote yaliyokukia.’ Kisha Rafaeli akatoweka, wasimwone tena. Basi, wakamsifu Mungu kwa nyimbo, wakamshukuru kwa ajili ya matendo yake makuu aliyowafanyia malaika wake Mungu alipokuwa amewatokea.”


Kumbe, kama huna kitabu hiki katika Biblia yako lazima ushindwe kujua na kukubali kweli mbili: mosi, kwamba malaika na watakatifu wanawasilisha sala mbele ya Mungu nao wanaripoti juu ya matendo yetu mema.


Kumbe, ni kwa sababu ya ukweli huu, Wakatoliki hawasiti kuwaomba malaika na watakatifu mbalimbali wawaombee kwa Mungu. Hapo ndipo zinapoingia sala na ibada mbalimbali kwa Bikira Maria AWAOMBEE wanadamu wote, wema kwa wakosefu, wazima kwa wafu.


Ukweli huu unaungwa mkono kwa kiashirio kizuri kilicho katika maombezi ya Maria kwa Yesu ili waliokuwa wanaishiwa divai wasaidiwe (soma Yn 2:1-12).


Pili, kwamba Bikira Maria, malaika na watakatifu hawaabudiwi isipokuwa kupitia kazi zao na maombezi yao Mungu anatukuzwa.


Hakika ukisoma vizuri Tobiti 12:11-21, utajua kwamba Bikira Maria, malaika na watakatifu hawaombwi kwa wenyewe bali wanaombwa wasimame kama waombezi wa wanadamu “wanaolimbana” na malimwengu haya yanayowachachafya.


Lakini kutokana na mtu kukataa jambo mahali fulani, hulazimika akatae popote na chochote kitakachoelekea kupindua msimamo wake. Kumbe, kanusho moja huzaa kanusho lingine hata kama ni kwa kulazimisha tu.


Ndiyo kisa basi, mtu anaposhuhudia mambo ya watakatifu kuwa na uwezo wa kuombea kwa kunukuu Ufu 5:8, 8:3-4, huwa kama anayechota maji kwa pakacha tu.


2. KWA KUKATAA KITABU CHA HEKIMA YA SULEMANI, lazima ukatae fundisho la Hekima (Roho Mtakatifu au Yesu Kristo) kuwa Nafsi ya Mungu kwa maana jambo hilo limeshuhudiwa na Hekima ya Sulemani 9: 6.9-12.


Hapa pameandikwa hivi:
“Hata kama mtu yeyote akiwa mkamilifu kiasi gani, bila Hekima atokaye kwako atakuwa bure tu. Hekima yupo pamoja nawe, naye ajua matendo yako, alikuwa pamoja nawe wakati ulipouumba ulimwengu.


Hekima anajua yanayokupendeza na yaliyo sawa kulingana na amri zako. Umpeleke, basi kutoka mbingu tukufu, kutoka kiti chako cha enzi kitukufu, ili akae nami na kufanya kazi pamoja nami, nipate kujifunza yale yanayokupendeza, maana Hekima anajua na anaelewa mambo yote, naye ataniongoza kwa busara katika matendo yangu, kwa utukufu wake atanilinda, hapo matendo yangu yatakubalika, nitawahukumu watu wako kwa haki na kustahili kuwa katika kiti cha enzi cha baba yangu.”


Basi, kama huna kitabu hiki katika Biblia yako lazima ushindwe kuujua na kukubali ukweli kwamba katika Mungu kuna Nafsi, Mwana na Roho Mtakatifu.


Kama hutakaidi kabisa basi utasema Yesu alikuwa ni mwanadamu mwema tu na Roho Mtakatifu nguvu za Mungu kutendea kazi tu. Huko ndiko kutakuwa kuzikana Nafsi mbili za Mungu kati ya tatu tunazopaswa Wakristo kuzikiri.


3. KWA KUKATAA KITABU 2 MAKABAYO, lazima ukatae uhalali wa kuwaombea marehemu kwa maana jambo hilo limeshuhudiwa na 2Mak 12:38-45.


Hapa pameandikwa hivi:
“Kisha Yuda aliwaongoza watu wake kwenda mjini Adulamu. Hiyo ilikuwa siku kabla ya Sabato, kwa hiyo wakajitakasa kadiri ya desturi ya Kiyahudi, kisa wakaadhimisha Sabato hapo.


Siku iliyofuata waliona ni harakia na muhimu kukusanya miili ya wenzao waliokuwa wameuawa vitani, na kuizika katika makaburi ya wazee wao.


Lakini katika kila maiti, walikuta zimefichwa nguoni sanamu ndogondogo za miungu iliyoabudiwa Yamnia, jambo ambalo sheria inawakataza Wayahudi kuzivaa. Hapo kila mtu alijua kwa nini hao walikuwa wameuawa.


“Hivyo, wakazisifu njia za Bwana, hakimu mwenye haki, afichuaye vilivyofichika na wakamwomba Bwana awafutilie mbali dhambi hiyo.


Kisha Yuda yule mtu mwadilifu, akawataka watu waepuke dhambi, kwa sababu walikuwa wamejionea wenyewe yaliyokuwa yamewapata wale waliokuwa wametenda dhambi.


Pia alichangisha kutoka kwa watu wake fedha ipatayo drakma elfu mbili akapeleka Yerusalemu kwa ajili ya dhabihu ya kuondolea dhambi.


Yuda alifanya tendo hilo jema kwa sababu aliamini juu ya ufufuo wa wafu. Kama asingekuwa na imani kwamba wafu watafufuliwa, ingekuwa ni upumbavu na kazi bure kuwaombea marehemu.


Lakinii akiwa anatazamia tuzo nzuri waliowekewa waliokufa wakiwa waaminifu kwa Mungu hilo lilikuwa wazo jema na takatifu. Kwa hiyo, Yuda alitolea dhabihu ya upatanisho ili wapate kuondolewa dhambi zao”.


Kama huna kitabu hiki katika Biblia yako lazima ushindwe kuujua na kukubali ukweli huu. Wakatoliki huwa tunawaombea marehemu si kwa sababu tunampelekea Mungu maombi mapya la hasha, ila kwa sababu sala zetu zilishajulikana na Mungu kabla mtu yule hajafa, wakati mtu anakufa na baada ya mtu yule kufa.


Mungu anayejua yaliyopita, yaliyopo na yajayo ndiye Mungu mwenyezi. Mungu asiyejua hivyo si mwenyezi, huyo ni sawa na Pd. Titus Amigu tu.


4. KWA KUKATAA KITABU CHA YOSHUA BEN SIRA, lazima ukatae mafundisho ya ulazima wa imani kuwekwa katika matendo kwa maana jambo hilo limekaziwa na kitabu kizima.


Kitabu hiki kilichokuwa kikitumiwa kama kitabu cha kiada mwanadamu anahimizwa aishi vyema maana ndilo deni kwa akili na utashi alivyopewa kwa kutofautishwa na wanyama wafugwao na hayawani wanaoishi kwa silika tu.


Yoshua ben Sira inazungumzia uzuri wa kuishi kiadilifu katika kila uwanja, malezi, kazi, urafiki, heshima, ndoa na kadhalika. Kumbe, kwa kukikataa kitabu cha Yoshua ben Sira sawa na Hekima ya Sulemani, lazima mtu akane umuhimu wa matendo katika kumtafuta Mungu naye ajikite zaidi kwenye misimamo ya “kwa neema tu” na “kwa imani tu” maana huna mafundisho mazuri juu ya matendo yaliyotukuka. Kumbe, hapo ndipo alipolazimika Martin Luther kuishia.


5. KWA KUTAA KITABU CHA YOSHUA BEN SIRA TENA, lazima ukatae mafundisho ya uhalali wa kunywa divai kwa wakati wake na kiasi chake kwa maana jambo hilo limeandikwa katika YbS 31:25-31. Hapa pameandikwa hivi:


“Usijioneshe kwuwa hodari wa kunywa mvinyo, maana mvinyo umewaangamiza wengi. Tanuru hupima ugumu wa chuma na mvinyo hupima mioyo ya watu katika shindano la wenye kiburi. Mvinyo ni kama uhai kwa mtu ukinywa kwa kiasi.


Maisha yafaa nini bila mvinyo? Imeumbwa iwafurahishe wanadamu. Kunywa mvinyo wakati wake na kwa kiasi, kwaleta shangwe moyoni na furaha rohoni. Lakini kunywa mvinyo kupita kiasi kunaleta kuumwa kichwa, uchungu na fedheha


Ulevi huongeza hasira ya mpuumbavu akajiumiza mwenyewe. Humdhoofisha na kumwongezea majeraha. Usimkaripie jirani yako kwenye mvinyo, wala usimdharau anapoifurahia karamu. Usimwambie neno la kumwonya wala umsimsumbue kwa kumtaka alipe deni”.


Kumbe, kama huna kitabu hiki katika Biblia yako, lazima ushindwe kuujua na kukubali ukweli wa kwamba divai si haramu ikinywewa kwa wakati wake na kwa kiasi.


Lakini, huu ndio ukweli uliomruhusu Yesu awe anakula na kunywa anapoalikwa na vile vile uliomruhusu awape watu waliokuwa kwenye sherehe ya harusi ya Kana divai (“oinos” siyo “gleukos”) ya kutosha.


6. KWA KUKATAA KITABU CHA YOSHUA BEN SIRA TENA, lazima ukatae fundisho la sakramenti ya Kitubio au Upatanisho kwa maana fundisho hilo limedokezwa katika YbS 5:4-7. Hapa pameandikwa hivi:


“Usiseme, ‘Nimetenda dhambi lakini nimepata balaa gani?’ Usitegemee kupata msamaha hata kuongeza dhambi juu ya dhambi. Usiseme, ‘Huruma yake ni kubwa, yaye atanisamehe dhambi zangu nyingi’.


Kumbuka, yeye ana huruma na ghadhabu na hasira yake huwakumba wenye dhambi. Usichelewe kumrudia Bwana wala usighairishe kurudi siku hata siku. Maana ghadhabu ya Bwana itakuwakia ghafla na wakati wa hukumu utaaangamia.”


Hali kadhalika, KWA KUKATAA KITABU CHA BARUKU, lazima ukatae pia fundisho la sakramenti ya Kitubio au Upatanisho kwa maana fundisho hilo limedokezwa vile vile katika Baruku 4:27-30. Hapa pameandikwa hivi:


“Jipeni moyo wanangu na kumlilia Mungu kwani yeye aliyewaleteeni jambo hilo atawakumbukeni. Kama vile mlivyokusudia kwenda mbali na Mungu vivyo hivyo rudini na kumtafuta kwa hamu mara kumi zaidi.


Hivyo, huyo aliyewaleteeni balaa hizi atawaokoeni na kuwaleteeni furaha ya kudumu milele. Jipe moyo, ee Yerusalemu, Mungu aliyekuita kwa jina lako atakufariji.”
Kumbe, kama huna kitabu cha Baruku katika Biblia yako, lazima ushindwe kuujua na kukubali ukweli huu kwamba Mungu alikusudia kuwaasisia wanadamu sakramenti ya Upatanisho au Kitubio.


Sakramenti hii ndiyo sakramenti inaiyotendea haki sadaka ya msalaba aliyoitolea Yesu kwa ufanisi mkubwa.


7. KWA KUKATAA KITABU CHA YOSHUA BEN SIRA TENA, lazima mtu ubaki katika utumwa wa kuamini ndoto hata baada ya Yesu kuufikisha ufunuo kileleni (Mk 9:7-8, Ebr 1:1-4).


Lakini neno la Mungu lasema ndoto zote ni upuuzi, isipokuwa zile zitokazo kwa Mungu tu (yaani zinazotokea mara kadhaa, kuwa na ujumbe maalumu na ujumbe wake kutopingana na mafundisho ya Kanisa). Jambo hili limeandikwa katika YbS 34:1-8.


Hapa pameandikwa hivi: “Mtu mjinga huwa na matumaini ya bure na ya uongo. Ndoto humpa mpumbavu mabawa ya kuruka. Kama mtu anayejaribu kushika kivuli na kufukuza upepo ndivyo alivyo mtu anayeamini ndoto. Ndoto ni kama kioo, sura inayoukabili uso.


Ni kitu gani kiwezacho kutakaswa na uchafu? Je, ukweli waweza kupatikana kwa uongo? Kupiga bao, ramli na ndoto ni upuuzi, akili huwa na mawazo kama ya mama anayejifungua.


Usizitie maanani ndoto isipokuwa kama zinatoka kwa Mungu Mkuu. Maana ndoto zimewadanganya wengi na wale wanaozitumaini wameaibishwa. Sheria ni kamili bila udanganyifu huo, nayo hekima ni kamilifu kwa mtu mwaminifu.”


Kumbe kwa kutumia Biblia ndogo, kwa maana ya kwamba isiyo na kitabu cha Yoshua ben Sira mwanadamu utaendelea na kusumbuka kutafuta maana ya kila ndoto. Zaidi ya hayo, utanunua vitabu vyote vinavyodaiwa kutafsiri ndoto za watu na hali kadhalika kuhangaika kuwaendea “wafasiri wa ndoto” wote ijapokuwa wenyewe ni waongo wasiojua jambo lolote la ajabu.


8. KWA KUKATAA KITABU CHA YOSHUA BEN SIRA TENA, lazima mtu ukatae uhalali wa dawa za asili hata kama zinatumiwa kwa uadilifu kwa maana jambo hilo limeandikwa katika YbS 38:1-14. Hapa pameandikwa hivi:


“Mpe daktari heshima anayostahili, kwa sababu ya huduma zake kwako, kwa vile naye aliumbwa na Bwana. Maana kipaji chake cha kuponya chatoka kwa Mungu Mkuu naye hupata zawadi kutoka kwa mfalme.


Ujuzi wa dakrari humfanya maarufu, naye huheshimiwa miongoni mwa wakuu. Bwana aliumba dawa zote kutoka ardhini na mtu mwenye nusara hawezi kuzidharau. Je, si kwa kijiti maji yaligeuzwa kuwa mazuri ili Mungu awaoneshs watu nguvu zake?


Bwana aliwapa watu maarifa na ujuzi ili atukuzwe katika kazi zake za ajabu. Kwa dawa huwapaonya watu na kuondoa maumivu, mchanganya dawa hutengeneza mchanyiko wake. Kazi za Bwana hazina mwisho, afya yote duniani hutoka kwake.


“Mwanangu, ukiugua usiwe mzembe juu ya ugonjwa, bali mwombe Bwana naye atakuponya. Acha makosa yako, uamue kutenda mema, na kutakasa moyo wako dhambi zote. Mtolee Bwana dhabihu ya harufu nzuri na dhabihu ya unga safi.


Umiminie dhabihu zako mafuta kadiri unavyoweza kupata. Kisha mengine mwachie daktari maana Bwana ndiye aliyemuumba; usikubali akuache maana unamhitaji. Kuna wakati ambapo kupona kuwategemea madaktari.


Maana nao pia wanamwomba Bwana ili awape mafanikio katika uchunguzi wao na katika kuponya ili kuokoa maisha. Mtu aliyetenda dhambi dhidi ya Muumba wake mwache aangukie mikononi mwa daktari.”


Kumbe, usipokuwa na Biblia yenye nukuu hii, utakuwa “unapinduka pinduka tikitaka” nyingi za kiakili kutaka kuhakikisha kwamba dawa za asili, kwa zenyewe, ni haramu.
Nakomea hapa.


Nadhani nimekujengea vyema hoja na kukutolea mifano mizuri kwamba makanisa mengine yana mungu mdogo kwa sababu ya kutumia Biblia ndogo. Kitendo cha kupunguza vitabu vya Biblia kutoka 72 au 73 hadi 66 kimetupa nje mafundisho mazuri ya Kanisa na kubana uelewa wa mafundisho yanayodumishwa na Kanisa Katoliki. Matokeo yake ya jumla ni kuzaliwa kwa mabishano endelevu kwa sababu ya kutofautiana vitabu vya rejea.


Na hili ni jambo la kawaida kama watu wanajadiliana jambo, tuseme la Fizikia, hawawezi kuelewana ikiwa mmoja anatumia muhtasari wa darasa la saba (yaani muhtasari mdogo) wakati mwingine anatumia kitabu cha Sekondari kwa mfano kitabu cha A.F.ABBOT.


Kumbe, mtu anayehama kutoka Kanisa Katoliki, Kanisa lenye Biblia kubwa na hivyo lenye Mungu mkubwa na kuhamia kanisa lenye Biblia ndogo na hivyo kujihusisha na mungu mdogo lazima ajiunge katika taabu ya kwanza kujielewesha na kishapo kuyatetea mafundisho madogo. Naomba mnipate uzuri. Kwa heri kwa leo pia!



Post a Comment