Ads (728x90)

Powered by Blogger.




Utangulizi
Kutokana na ufunuo wa kimungu twafahamu na kujua kwamba mtu yupo duniani ili amjue Mungu, ampende, amtumike na halafu afike mbinguni. Haya ndio madhumuni ya kweli na thabiti ya uwepo wa mtu, binadamu na historia.

Ni jambo la kusikitisha sana kuona kwamba kuna watu wengi ambao hawajitambui hata kidogo, kwa nini wapo hapa duniani. Watu hao wapo pia kwenye kundi la Wakatoliki. Sasa hivi sisi binadamu tunaishi katika utamaduni ambao kwa kiasi kikubwa umeegemea zaidi katika mambo ya kidunia. 

Kuna mamilioni mengi ya watu walio ndugu zetu na jamaa zetu na wanaomsadiki Mungu na wangependa  kuona malimwengu yasiwe na nafasi kumtawala binadamu, lakini sauti yao haina nguvu wala haisikiki katika utamaduni wa kawaida.

Mkazo mkubwa karibu hata nguvu zote katika vyombo vya habari…. Radio, Tv (Runinga) n.k…… hivyo vyote vipo katika dunia hii. Ndio maana mkazo mkubwa unaelekezwa katika masuala ya kifedha, ngono, heshima, siasa, nguvu na uwezo wa kiserikali.

Watu wengi wanaona kumcha Mungu ni suala lililopitwa na wakati, linawapotezea muda wao na pengine huwacheleweshea maendeleo yao.  Ebu tujifunze kwa waisraeli ambao waligundua kwamba uchaji wa Mungu ni mwanzo wa Hekima.


Taifa la Israeli na utafutaji wa Hekima ya kweli
(a)Waisraeli na vitabu vyao vya Hekima

Waisraeli ni kati ya mataifa makubwa katika historia ya ulimwengu, walikuwa na “hekima” yao, kwa mujibu wa maelezo yaliyopo tukiruhusiwa kutamka vile ambavyo inaelezwa katika vitabu vitano vya Agano la Kale katika Biblia. 

Kwa hiyo vitabu hivi vinaitwa “Vitabu vya Hekima” navyo ni Ayubu, Mithali, Mhubiri, Yoshua bin sira na Hekima ya Sulemani.

(b) Waisraeli Waliamini

Waisraeli waliamini kuwa hekima ya kweli ni ile ambayo mtu anaweza kuitumia hasa katika maisha ya kila siku. Pamoja na Wamisri wa zama hizo, wao waliona kuwa mtu mwenye hekima ni yule anayeweza kutekeleza maisha yake, siku kwa siku pamoja na taabu na matatizo yake kwa ustadi pasipo kumuudhi mwingine. Tena tukikaza waliamini kuwa hekima ni ile inayoweza kutumika na wala si kuijua tu katika nadhiri mbalimbali.

Basi, tukisoma vitabu hivi, tunaona maonyo mbalimbali  ambayo kwa lugha ya leo tungeliweza kuyaita kama mwongozo. Mwongozo huo unahusu maisha ya kila siku, ili mtu akifuata, aweze kutekeleza maisha yake ya kila siku pamoja na matatizo yake kwa ustadi au ufundi unaotakiwa.

(c)Mambo madogo madogo

Maonyo yaliyoandikwa katika mfumo huo yanahusu mambo ya kila siku, na mara nyingi mambo madogo madogo. Labda msomaji unaweza kuuliza: kwa nini kutoa mwongozo au maonyo katika mambo madogo madogo ya kila siku? Waisraeli walitambua kuwa matendo hayo madogo madogo ya kila siku ndiyo yanayofanya maisha ya watu wengi.

Wao walijua, ijapo sisi siku hizi tunasahau  kuwa maisha ya binadamu yanajengwa na kuundwa na matendo ya kila siku kama vile kutembea, kuongea na watu wa aina mbalimbali, uhusiano na watu wa aina mbalimbali, shughuli za nyumbani na hata sokoni; kifupi  tungelisema wajibu wa kila siku hata ukiwa mdogo kiasi gani.

Kwani ni dhahiri kwamba matendo makubwa au ya kishujaa si sehemu ya maisha ya kawaida kwa watu wengi.

Aidha tusisahau kuwa hata katika mambo madogo madogo mtu anaweza kukosa raha na amani moyoni iwapo mambo yanamwendea mrama.

Labda wasomaji wa Biblia wamecheka au walau kutabasamu mara nyingi waliposoma sentensi nyingi katika vitabu hivi vya hekima, kwani vyaeleza mambo ambayo mara nyingi watu hawajali katika maisha kwa mfano twasoma: 

“Midomo ya malaya hudondoza asali, na kinywa chake ni laini kuliko mafuta” Mithali 5:3 au mtu anayezungumza pamoja na mpumbavu amefanana  na yeye anayezungumza na mwenye kusinzia mwishowe atasema, Nini?”. Yoshua bin Sira 22:10.

Hata tukitabasamu tusomapo sentensi kama hizo, yatupasa tukumbuke kuwa yote yaliyoandikwa katika Biblia yameandikwa ili kutufundisha sisi, hata kizazi chetu cha leo. Na mtume Paulo alikazia jambo hili alipowaandikia wakristo wa Korintho (Taz. 1Kor. 10: 1-11).
(d) Msingi wake
Lakini mtu atapata wapi nguvu ya kuweza kutekeleza maisha yake kwa ustadi huo unaotakiwa? Tena msomaji utauliza jambo hili linawezekanaje kwetu ambao tuna matatizo mengi na pengine ni tofauti kabisa na yao?.

Vitabu vya Hekima vyatutatulia tatizo hilo. Kwa vile hekima ya kweli ni kuweza kutekeleza maisha ya kila siku pamoja na matatizo yake, kiini cha kuweza kutekeleza maisha yake ya kila siku huyu ana hekima.
Yeyote asiyeishi kadiri ya matakwa au sheria za Mungu, hawezi kuwa na hekima hiyo kwani wao waliamini kwa dhati kuwa kumcha Mungu ni chanzo na msingi wa kupata hekima.

Kwa sababu hiyo waliandika: “kumcha Mungu (Bwana) ndio mwanzo wa hekima, wote wafanyao hayo wana akili njema” (Zab 111:100 au wazi zaidi: “Hekima yote ni kumcha Bwana (Yoshua bin Sira 19:20).

(e) Walipitia Taabu

Tuulize walipataje kuamini jambo hili? Sote twajua kuwa Waisraeli walikuwa taifa teule la Mungu. Hata hivi Mungu aliwapeleka utumwani Babeli wakatawaliwa na kuwatumikia watu wasiomjua Mungu wa kweli “washenzi”.

Baada ya kuwa watumwa huko Babeli na kupata taabu nyingi, waisraeli waliamini jambo hili kikamilifu. Kwani, baadaye walijua ni kwa nini Mungu aliwapeleka utumwani kuwa chini ya wapagani yaani “washenzi” ndivyo walivyowaita  wote wasiokuwa wayahudi.

Walipelekwa utumwani kwa sababu za kumwasi Mungu, na hivi Mungu hakuwahurumia eti kwa kuwa ni taifa  lake tukufu kama wenyewe walivyotumaini.
Kutokana na taabu  hizo baadaye waliamini sana kuwa kumcha Mungu ndiyo hatua ya kwanza kabisa ya kujipatia hekima ya kweli. 

Huko kumcha Mungu sharti kuwepo daima, katika kila jambo analolifanya mtu.

Hata katika kujenga nchi, katika maendeleo sharti kumjali Mungu. Kazi za kila siku na juhudi za mwanadamu sharti zipate baraka na uongozi wa mwenyezi Mungu, vingine ni bure.

Bwana asipojenga nyumba, waijengao wafanya kazi bure, Bwana asipoulinda mji, yeye aulindaye akesha bure (Zab 127:1) ndivyo walivyoimba na kusali watu walioitwa Waisraeli. 

(e) Kinyume chake Je?

Iwapo kumcha Mungu, kutenda na kuishi kadiri anavyotaka Mwenyezi Mungu ni kiini cha kupata hekima, kutomcha Mungu ni nini? Waisraeli walimwona mtu asiyemjali Mungu ni Mpumbavu au mjinga (Taz Zab. 14 na 53). 

Ujinga au upumbavu huo unafikia kilele chake pale mtu huyu anapotenda uovu fulani au dhambi. Mtu asiyemjali Mwenyezi Mungu akatekeleza maisha yake kama anavyotaka mwenyewe tu huyu hana hekima, hata kama angelionekana machoni pa wengine kuwa ana akili nzuri. Maana kumcha Mungu ni Mwanzo wa Hekima.

Tena kazi ya mtu wa namna hii, hata kama zingalionekana kuwa vema, mwishoni zitaangamia tu, kwani kazi hizi zitapata wapi baraka ya Mungu iwapo huyu mtu hamjali Mwenyezi Mungu?.

(g) Leo Je?

Tungeliweza kuendelea kuitazama hekima hii ya kweli ambayo Waisraeli waliiamini. Hekima hiyo ndiyo inayotakiwa wakristo tuizingatie na kutoa mwanga  kwa wengine wasioijua bado.

Kwani mtu akiwa na fikira au mawazo kuwa dini ni kasumba na kusema eti dini inazuia maendeleo ni vigumu kuamini kuwa anajua maana halisi ya dini.

Tena, wakristo tunaamini kuwa Biblia  ni neno la Mungu na ndivyo ilivyo. Kumbe, Biblia hutufundisha hekima ya kweli ni nini  kwa hiyo si waisraeli wanaotufundisha wao waamini, bali ni Mungu mwenyewe atufundishaye jambo hili.

Tukitaka kufanikiwa katika shughuli zetu sharti la kwanza si juhudi zetu, bali kutenda kama anavyotaka Mungu na kumwomba baraka kwa kazi. 

Maana utaalam pasipo baraka za Mungu hautoshi. Hata siku hizi, twaweza kufundishwa mengi, mradi tu tukifungua Biblia na kusoma walau kidogokidogo.

Binadamu na utafutaji wa hekima ya Mungu
(a)Mtu wa leo huitwa “Mtu Mwenye Hekima”

Wataalamu wa Sayansi ya Anthropolojia ya kimwili (Physical Anthropology) Sayansi ambayo huchunguza habari za uhai wa mtu, historia yake katika mageuzi yenye kuendelea (evalution) uhusiano wake na viumbe wengine walio karibu naye n.k. 

Hutuambia kwamba mtu, jinsi alivyo sasa, hakutokea duniani ghafla bali ana historia ndefu. Amebadilika polepole kwa njia ya mageuzi yenye kuendelea na kupata hali yake na umbo lake la leo (Theory of Evolution).

Mtu wa sasa huitwa kwa kilatini “Homo Sapiens” yaani “Mtu Mwenye hekima”. babu yake wa kwanza ajulikanaye kwa sasa “Homo Habilis” maana yake “Mtu mwenye kuweza” mabaki yake yamepatikana huko Olduvai Gorge Tanzania ambapo aliishi kama miaka 1, 250, 000 – 1, 750, 000 hata pengine na zaidi iliyopita.

Mtu huyo aliye babu alijua kutumia vifaa, fulani kama kisu kilichotengenezwa kwa jiwe hivyo wataalam wakampa jina hilo la mtu “Mwenye kuweza”.

“Mtu wa sasa kama tulivyosikia huitwa Mtu mwenye hekima yaani wewe na mimi basi mtu aliye mkristo awe makini zaidi kwa vile anatazamwa kuwa ni mwenye hekima ili amche Mungu vizuri.

(b)Maana ya neno Hekima

Kama tumefuatilia maelezo ya neno “hekima” kama Waisraeli walivyoelewa hapo juu na pia wataalam wa elimu ya Anthropology  wanavyodiriki kumwita mtu wa leo kwa jina la “Homo sapiens yaani” mtu mwenye Hekima.

Basi kadiri ya matumizi ya neno hekima katika Biblia hali kadhalika katika matumizi yake nje ya Biblia hali “Hekima” ni elimu au mbinu zinazomwezesha mtu kuyamudu maisha yake ya kila siku.

Hata ufundi wa msanii huitwa “Hekima” pia (Kutoka 31:1-5) hali kadhalika uwezo wa kutawala vizuri ni hekima, kama hekima aliyojaliwa Solomoni (1 Wafalme 3:1-15). 

Hekima ni Elimu inayomsaidia mtu kutafuta majibu kwa matatizo ya kila siku kwa mfano Mbinu za kuhusiana vizuri na watu wa matabaka mbalimbali hizo zinapatikanaje? Mang’amuzi ya maisha humpa mtu mbinu hizo.

Wale waliopata mang’amuzi ya maisha hurithisha elimu kama hiyo inapatikana katika jamii zetu za wanadamu ispokuwa siyo jamii zote za wanadamu zimewahi kuaandika elimu hiyo. Katika jamii zisizokuwa na maandishi hekima hizo zimo katika methali na vitendawili.

(c)Hata maana ya neno Falsafa limetokana na neno hekima

Falsafa (Philosophy) ni neno litokanalo na maneno mawili ya Kigiriki yenye maana ya Upendo na Hekima kwa hilo neno falsafa linamaanisha  upendaji wa hekima katika mambo yote na kushirikiana na ukweli huo. Falsafa  huanza kwa njia ya mshangao yaani Falsafa hukiona kile kitu kionekanacho cha kawaida  kama ni cha kushangaza na kitu cha kushangaza, kwetu sisi falsafa hukiona ni cha kawaida tu. 

Falsafa inakufanya uwe huru kifikra na kujitegemea kimawazo na kimaoni.

Binadamu asiyekuwa na falsafa yoyote humfanya aonekane hana faida katika jamii. Falsafa humsaidia mtu kushinda ndoto zake za mambo fulani. Ni kweli kuwa jinsi kila mmoja anavyofikiria hutegemea jamii, elimu, mazingira utamaduni, dini, uchumi, tabia na siasa inayomzunguka, lakini falsafa inamsaidia  mtu kwenda juu zaidi ya haya yote.

Falsafa inashughulika na mambo makuu matatu yaani Mungu, binadamu na dunia. Falsafa humsaidia mtu kuwasilisha mawazo yake katika mtiririko wa mawazo mantiki unaoeleweka kwa wenzake.

Falsafa ni Elimu inayojihusisha na ukweli kama ulivyo. Na kwa sababu hii elimu inajihusisha zaidi na masuala ya msingi ya kila kitu na kanuni ya uwepo.

(d)Hekima inayofaa ni ile inayomheshimu Mungu

Ni mapenzi ya Mungu kwamba wanadamu wajifunze na kukuza hekima ya maisha, ili waweze kuishi kwa maarifa ya kweli. Kwa njia hii maisha yao yanafaa, yakimfurahisha Mungu na kunufaisha maisha yao na yale  ya watu wengine (Mit 1:2-7, 2:7-11, Efe 5:15-16). Hekima inayofaa ni ile inayomheshimu Mungu.

Hekima inayopendekezwa katika Biblia inahusika zaidi na mambo yanayosaidia maisha ya kila siku kuliko mawazo ya Falsafa (Philosophy) tu watu wanaishi katika ulimwengu wenye matatizo, wanapaswa kuishi na watu wenye matatizo (Kumb 1:13-15, 34:9, 1Fal 3:9, Mdo 6:3,7:10) lakini msingi wa hekima ile si ujanja wa binadamu, bali ni utii na heshima kwa Mungu.

Mungu ni asili ya hekima ya kweli, naye  anawapa watu wale wanaoitafuta (Mit 1:7, 2:6, 9:10, Dan 2:20 Rum 16:27, 1Kor 1:30, Yak 1:5-8).

Bila heshima ile, hekima inaweza kuwa ya ubinafsi au ya kidunia, inayoonekana katika udanganyifu. Hekima isiyomjali Mungu ni kama vile tabia ya wivu na udanganyifu.  Kinyume chake hekima itokayo kwa Mungu alama yake ni unyenyekevu, unyofu na hamu ya kusaidia watu (Mit 8:12-16, 10:8, 11:2, Isa 5:21, Yakobo 3:13-18).

Hekima hii itokayo kwa Mungu inapatikana kama watu wako tayari kuacha ujinga wa njia zao za ubinafsi na kuipokea kutoka kwa Mungu (Mit 1:20-23, 8:1-6, 9:1-6) inawataka watu washinde majaribu ya maisha (Mit 6:23-27) lakini wakiikataa watajipatia aibu na hali ya kukatisha tamaa (Mit 1:20, 24-26, 5:11-13, 7:1-23, Mhu 10:1-3).



Post a Comment