Ads (728x90)

Powered by Blogger.




-Marejea yanazalisha magunia 68  kwa hekta moja
-Baba wa Taifa alikuwa ni mfuasi mkubwa wa marejea

Na Albano Midelo

Kilimo ni Mwajiri Mkuu wa watanzania kutokana na takwimu kuonesha kuwa asilimia zaidi ya 75 ya watanzania wamejiajiri katika sekta ya kilimo.

Sekta ya kilimo nchini inakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo ya wakulima wengi kuendelea kutumia jembe la mkono,bei ya  kubwa ya pembejeo na ukosefu wa soko la uhakika la mazao.

Hata hivyo uchunguzi umebaini kuwa tatizo la kutegemea mbolea za viwandani linaweza kumalizika au kupungua iwapo kitafufuliwa kituo cha mradi wa mbolea ya kilimo mseto (marejea) kilichopo Peramiho Halmashauri ya  Wilaya ya Songea Mkoa wa Ruvuma.

Kituo cha MRUMA Peramiho ndiyo Kituo pekee katika nchi nzima ambacho kilikuwa  kinazalisha mbegu za mbolea ya marejea kilichokuwa chini ya Kanisa Katoliki Abasia ya  Peramiho ambacho  kimekufa tangu mwaka 2013.

Hivi sasa majengo Kituo hicho yanatumiwa kama hosteli ya kulala wanachuo wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Madaktari cha Bugando tawi la  Peramiho.

Historia inaonesha kuwa kilimo mseto kwa kutumia mradi wa kurutubisha ardhi kwa kutumia mbolea ya marejea kituo cha MRUMA Peramiho  kilianza tangu 1942.

Mwanzilishi wa mbolea ya marejea ni padre Otmar na Bruda Krisp OSB ambaye aliyaokota marejea kutoka porini na kuhamasisha watu kutumia kama mbolea mbadala.

Mwaka 1963 bruda Herman OSB  wa kituo hicho  alianza kutumia mbolea ya marejea na kulishia mifugo ambapo mwaka 1983 ilianzishwa benki ya mbegu za marejea Peramiho (sunnhemp seed bank).

Mwaka 1987 baada  ya kuona umuhimu wa marejea katika kurutubisha ardhi kilianzishwa rasmi kituo cha mradi wa kurutubisha  udongo kwa kutumia marejea  Peramiho (MRUMA) kituo ambacho kilikuwa kinatoa elimu ya kutumia mbolea ya marejea kwa wakulima katika nchi nzima.

Gabriel Mhagama aliyekuwa Mkuu wa Kituo cha MRUMA hadi kinakufa mwaka 2013  anasema kuna mimea mingi ambayo ina uwezo wa kuongeza rutuba katika udongo  ikiwemo   mimea jamii ya kunde.

Mhagama anasema alikabidhiwa kuwa Mkuu wa Kituo hicho tangu mwaka 1991 kutoka kwa muasisi wa Kituo hicho hayati Padre Gerald ambaye alifariki dunia mwaka 2000 ambapo hivi sasa wataalam wengi wa masomo ya kilimo kutoka ndani na nje ya nchi wamekuwa wakifika katika Kituo hicho kufanya utafiti na kutunukiwa shahada za kwanza,shahada ya uzamili(masters) pili na wengine wametunukiwa shahada ya uzamivu (PHD).

Hata Mhagama anasema utafiti uliofanywa katika Kituo cha MRUMA tangu mwaka 1942 umebaini kuwa mimea ya porini aina marejea inachukua nafasi ya kwanza kwa kurutubisha ardhi na mkulima akitumia mbolea hiyo ana uwezo wa kuzalisha mazao mara dufu zaidi ya kutumia mbolea za viwandani.

Utafiti uliofanywa na kituo cha kilimo Uyole kuhusu mbolea ya marejea ulibaini kuwa shamba la hekta moja  lililolimwa marejea mwaka uliotangulia linaweza kutoa magunia 68  ya mahindi yenye uzito wa kilo 100 badala ya magunia 14 tu iwapo haujatumia marejea.

Anasema baada ya kupandwa na kuota ni lazima kufyeka marejea baada ya wiki mbili hadi  mwezi mmoja na kuyageuza kwa kuchanganywa na udongo ili yaoze iwapo unataka kulima mazao katika shamba hilo ndani ya mwaka huo.

“Iwapo unataka shamba lililopandwa marejea, kulima mwaka unaofuata unatakiwa kuyaacha marejea yakue hadi yatoe mbegu’’,anasisitiza Mhagama.

Utafiti umebaini kuwa mbolea ya marejea ndiyo majibu ya mkulima ambaye hawezi kumudu kununua mbolea ya viwandani kwa kuwa mbolea hiyo  hurutubisha na kudumisha rutuba ardhini.

“Siku zote tunawambia watu kwanini wanang’ang’ania kulima mazao kwa kutumia mbolea za chumvi chumvi wakati zinawaumiza na kuua ardhi,badala ya kuchukua mbolea ya marejea ambayo hayana gharama”, anasisitiza Mhagama.

Kulingana na mtaalam huyo  mbolea ya marejea husaidia wiki mbili hadi mwezi mmoja baada ya kufyeka shamba  ambapo mkulima anatakiwa kupanda marejea kilo 20 kwa ekari na kutumia mfumo wa kubadilisha mazao yaani crop rotation ili kupata mafanikio wakati wa kutumia mbolea ya marejea.

Uchunguzi umebaini kuwa miaka ya 1983 mbolea ya marejea ilianza kutumiwa na wakulima wengi katika sehemu mbalimbali nchini ambapo wakulima na vikundi vya wakulima walifika katika Kituo cha MRUMA Peramiho kujifunza kuhusu uzalishaji wa mbolea hiyo  hali ambayo ilisababisha maelfu ya tani za mbegu za marejea kununuliwa na kwenda kuzalishwa.

Aliyekuwa Mkuu wa Kituo cha MRUMA Gabriel Mhagama anasema miaka ya 1980,Baba wa Taifa hayati Mwalimu Julius Nyerere alitembelea kituo hicho na kufurahishwa na uzalishaji wa mbolea hiyo hali iliyosababisha baba wa Taifa kununua tani za mbegu za marejea na kununua vitabu mbalimbali vinavyotoa elimu ya mbolea ya marejea.

“Padre Gerodi masisi wa marejea na hayati Baba wa Taifa walikuwa ni wafuasi wakubwa wa mbolea ya marejea ambapo mama Maria Nyerere bado anaendelea kutumia mbolea ya marejea, mwaka 2012 alinunua tani mbili za marejea ambazo tulimpelekea  nyumbani kwake Butihama”, anasisitiza Mhagama.

Mhagama anasema kuwa marejea kutoka Peramiho yameenea karibu nusu ya Bara la Afrika na mengine yamepelekwa hadi katika Bara la Ulaya ikiwemo nchi ya Uswis ambapo nchi hizo zinatumia vitabu vya mafunzo ya mbolea hiyo na kufanya kilimo hicho kuwa endelevu.

“jambo la kusikitisha ukiachia aliyekuwa Mkuu wa Mkoa Mstaafu wa Ruvuma hayati Dk.Lawrence Gama, baba wa Taifa na Mke wake mama Maria Nyerere ambao wametembelea kituo chetu,hadi kituo kinakufa mwaka 2013 hakuna watalaam wa ugani wa serikali Mbunge,Mkuu wa Mkoa,Mkuu wa Wilaya,Waziri wa Kilimo wala Rais aliyetembelea hapa “,anasema Mhagama.

Mhagama anasema hayati Dk.Gama akiwa Mbunge wa Songea Mjini alipeleka teknolojia ya mbolea ya marejea bungeni ili Waziri wa Kilimo aweze kufuatilia zaidi kuhusu matumizi ya mbolea hiyo na kwamba jambo la kusikitisha tangu wakati huo hadi sasa hakuna ufuatiliaji wowote wala hatua za kuhakikisha wakulima nchini wanahamasishwa kutumia mbolea ya marejea.

Mtaalam huyo anasema dhana ya kilimo kwanza ambayo ilipigiwa chapuo na Rais Mstaafu Jakaya Kikwete na Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda ingeweza kupata mafanikio makubwa endapo watanzania wote wangetumia mbolea ya marejea ambayo ni endelevu kwenye udongo.

“Serikali ingenipa nafasi hata ya saa moja katika Bunge la Muungano ningeweze kutoa elimu hii kwa wabunge wote naamini wabunge wangehamasisha wapiga kura wao kuachana na mbolea za viwandani na kuanza kutumia mbolea ya marejea”,anasisitiza Mhagama.
   
Naye Mwakilishi kutoka Shirika la Tanzania Organic Agriculture Movement (TOAM) Noel Kwai anasema  kilimo hai sio kitu kigumu kwa sababu Mkulima wa kawaida anaweza kutumia mbolea za asili ambazo ni endelevu na hazina madhara kwenye udongo.

“Historia inaonesha kuwa Kilimo Hai kimeanzia Peramiho ambako waligundua mbolea ya marejea  ”,anasema Kwai.

Albano Midelo ni Mchangiaji wa gazeti hili unaweza kuwasiliana kwa simu 0784765917,baruapepe albano.midelo@gmail.com



Post a Comment