Ads (728x90)

Powered by Blogger.


Utangulizi:

Image result for UCHAWI AU USHIRIKINAUchawi kadiri ya imani ya kipagani ni nguvu isiyoumbwa na Mungu wala haitambuliwi na Mungu, nguvu hiyo inadhuru watu kwa namna mbalimbali. Wanaotumia nguvu hiyo wanaitwa Wachawi.
Kuna watu wanajisifu kwamba wanaweza kukinga au kuzuia uchawi wao wanaitwa waganga wa uchawi. Mara ngingi sana waganga hao ni wahongo na wanajipatia mali za watu kwa udanganyifu au uelevu wao.
Kwenye uchawi mara nyingi sana watu wabaya hujificha na kuingiza maovu yao wanayowatendea wenzao huku wakisema: “huo ni uchawi” kumbe ni watu wanatumia sumu na kuua watu wengine kwa sababu ya hasira zao au kwa sababu wameajiriwa ili kupata fedha.
Baadhi ya watu huapiza wengine na hata kuwajulisha kusudio lao kwa kuwahofisha wengine ili mwisho wake wafe kwa hofu ile, wakati mwingine wanaitwa walozi ndiyo aina mojawapo ya uchawi. Lakini ulozi wenyewe kamwe haupo bali ni mitego tu! inaweza ikawa ni sumu tofauti na uchawi.
Waovu wanajificha  katika ulozi kumbe wana tumia sumu ili kuwadhuru wengine. Wengine husema kwamba kwa uchawi wao uingia wanyama wakubwa na kwa nguvu zao huharibu mifugo ya watu, hata kuua watu wenyewe.
Maneno hayo ni njia ya kuficha maovu yao. Mtu hawezi kuingilia mnyama ama kugeuka Simba au Chui haiwezekani. Lakini kuna watu wenye akili sana wajuao kutafuata mizizi, hata dawa zingine za majani zinazotoa harufu kama jike la mnyama mkali wakati wa kupandwa.
Watu huo huficha dawa hiyo karibu na nyumba ya adui wao na usiku dume wa aina ya mnyama hufika na kulitafuna jike lake kwa kuwa halimwoni, hupata hasira na kuleta matata hata kuua mifugo au hata watu wa eneo husika.
Ni wazi kwamba watu watendao mambo hayo, yaani “aina zile za uchawi” ni waovu sana na Mungu atawaadhibu kadiri ya matendo yao. Lakini hata wanaosadiki mambo hayo  humkosea Mungu, sababu husema kuwa katika mambo mengine – kama uchawi – Mungu hataki kuzuia maovu hayo ama hawezi kuyazuia. Basi, hivi humkatalia Mungu  sifa na Enzi yake wema wake na hasa kukana maongezi yake ya milele.
Kila Mkristo akumbuke sana neno hili “palipo imani chache ushirikina ni mwingi” kama mtu ana imani iliyoimara  na kumsadiki Mungu atamwamini pia Mungu kwa moyo wote na hataelekea upande wa ushirikina na mambo mengine mabaya ya kipagani.
Watu na tamaa ya kutumia nguvu za ajabu au nguvu za giza
Tangu nyakati za kale watu walikuwa wakitamani kutumia nguvu za ajabu kama vile uchawi au kupiga ramli au bao ili kuwasaidia kutabiri mambo yaliyowakabili. Kutabiri kwa namna hiyo mara nyingine uitwa “uaguzi” (Mdo 16:16-18).
Uganga au uchawi huwa na maana zaidi kuliko  kutafuta ubashiri tu, jaribu kutumia nguvu za uchawi ili kuongoza matukio yajayo. Uganga huo mara nyingine una makusudi mabaya ukiwakabili maadui kwa njia ya laana, kusihiri na matendo ya sherehe fulani ya uchawi.
Mara nyingine sehemu ya makusudio yake inaweza ikawa njema mtu akijaribu kugeuka au kugeuza au pengine hata kubatilisha laana au uchawi fulani (Hes 24:1, Isam 6:2, 2Fal 17:21, 6, Dan 2:2, Ufu 9:21).
Lakini uaguzi na uchawi huchukua nguvu yake kutoka mashetani (Majini) wa ulimwengu wa kiroho, kwa sababu hiyo mafundisho ya Kanisa Katoliki na Biblia hulaumu na kukataza mambo haya kabisa (Law 19:26, 31. 20:6, 27, Kumb 18:10-11, 2Fal 21:6, 23:24, Gal5 :19-20, Ufu 9:21, 21:8, 22:15) wachawi wanatumia nguvu zao kinyume na Mungu kwa makusudi.
Uaguzi na uchawi
Baadhi ya njia za uaguzi kwa mujibu wa Biblia ni pamoja na kutupa mishale hewani na kuangalia alama zilizoonekana ulipoangukia (Eze 21:21), kutazama maini ya mnyama aliyechinjwa  kwa ajili ya sadaka (Eze 21:21), kuuliza roho za watu waliokufa (Isam 28:8-9). Kuchunguza kusogea kwa nyota angani (Isa 47:13).  Kutazama katika chombo kikubwa cha Maji (Mwa 44:5, 15) na kuua watu (Eze 13:17-19).
Waaguzi walikuwa miongoni mwa washauri wakuu wa mfalme wa nchini nyingi za kale (Kut 7:11, Dan 2:2). Uaguzi, uchawi na mambo mengine ya aina hiyo ni kinyume cha njia za Mungu sio tu kwa sababu mambo hayo yanapata nguvu zake katika mashetani yaliyo maovu, bali pia nguvu hizo na mambo yote hayo hukanusha imani ya Kikristo.
Uchawi na ushirikina ni Unajisi wa Roho
Uchawai au ushirikina ni unajisi wa Roho na ni zaidi ya ujinga. Ni ibada mbaya sana ya sanamu ya kujisalimisha si kwa vitu bali kwa Ibilisi mwenyewe. Kwa kujiweka mikononi mwake ukimtumainia wakati wote.
Ni kuamua kuamini na kutumaini nguvu za giza na kudharau nguvu za Mungu. Kukubali kuamini na kutumia nguvu za giza kwa jambo lolote lile kwa mkataba maalumu na shetani.
Sababu za watu kujishirikisha katika ushirikina unaomilikiwa na shetani ni tatu: mbili zipo upande wa wateja (wajinga) na moja ipo upande wa Waganga (Wajanja), kwa wateja ni uhaba wa imani na ujinga.
Kwa waganga (wajanja) ni mradi wa kutapeli ili kujipatia mali, vitu na fedha kwa njia ya udanganyifu. Ni kweli kwamba shetani ana nguvu lakini nguvu zake ni haramu zenye kuharibu na kuangamiza na zina mipaka yake.
guvu zake ni zenye kudhuru roho na hata mwili wa mteja wala sio za kujenga hata kidogo. Wajinga ndio wanaoamini mambo ya ushirikini, wajinga wana  uhaba wa imani, wakiamini kwamba kila jambo baya au ovu maishani husababishwa na watu wengine kichawi.
 Kwa ujinga wao hawawezi kuamini kuwa magonjwa husababishwa na viini mbali mbali vya magonjwa husika, kama vile bacteria, minyoo, virusi n.k. hata wanapoelimishwa juu ya njia mbali mbali za kujikinga na maambukizi hupuuza na hawaanini.
Enzi za ulimwengu wa giza ushirikina ulithaminiwa sana. Ulikuwa mradi mzuri uliweza kufundishwa hata mashuleni na kulikuwa na vitabu vya kufundishia. Dini nyingine zisizo za Kikristo huthamini mambo hayo hadi sasa.
Kitendo hicho kwa Kristo ni kufuru kwa Mungu. Lakini Mungu amejifunua kwetu sisi wakristo kwa njia ya Bwana Wetu Yesu Kristo aliye njia ya ukweli ya uzima (Yoh 14:6).
Maonyo ya Mungu dhidi ya nguvu za giza
Mungu ametuonya dhidi ya nguvu hizi za shetani na utapeli. (Yer 1:10) kwa midomo ya manabii alionya watu dhidi ya shughuli zote za kichawi (Isa 8:19-20, Eze 13:18, Malaki 3:5, Kumb 19:9-14, Fal 23:24, Law 19:26-29, Isaya 4415:23, Mk 5:12, Jambo hili ni ubatili Isaya 44:25, ni uongo (Eze 21:19, Zek 10:2).
Adhabu ya wenye kuwaendeleza wachawi katika Biblia upande wa Agano la Kale watu wote waliwaendea wachawi upande wa uganga walitengwa na jamii (Kut 22:18, Law 20:6-7)
Kwa yule aliyeshughulika na ushirikina adhabu yake ilikuwa ni kifo, tena bila huruma (Kut 22:18, Isam 28:3,9, Mika 5:12) katika Biblia wapo wengi walioshughulika na uchawi: Wamisri (Isa 19:3) wachawi wakati wa Farao (Kut 7:11,22,8:7, 18).
Balaam (Hes 22:6, 23:23) Yezebel (2Fal 9:22), Wanajimu (Yer 10:2, Mik 3:6-7) Manabii wa uongo Yer 14: 27:9), Elima – Ber Yesu (Mdo 13:4-12) Simon Mchawi (Mdo 8:9, 11), Wayahudi Watembezi (Mdo 19:13) wana wa sweva (Mdo 19: 14), Manabii wengine wa uongo Mt 24:24) Mwaguzi wa Filipi (Mdo 16:16).
Hitimisho
Bwana Yesu alishinda nguvu zote za uovu wa shetani na katika yeye waumini wanaweza kushinda (Ef 1:19-21, 2:6, Kol 2:8-10, 3:1-3). Wanaamini nguvu hiyo kana kwamba ni aina nyingine ya uwezo wa uganga (Mdo 19:13-16).
Wanaojiusisha na ushirikina Mtume Paulo amewaorodhesha katika kundi moja na Waasherati, Walevi, walafi, wafisadi, wauaji n.k. (Taz Gal 5: 19-21, Ufu 22:14,15. Mambo hayo ni imani ya kusadikishwa tu katika progaramu ya ubongo wetu.
Dawa pekee kwa wanaamini wa imani za kijinga (ushirikina) ni kuwapa elimu ya imani, sala, tafakari ya neno la Mungu kuboresha mara kwa mara uchumi na miundombinu yake hasa kwa upande wa afya na usafiri. Vile vile kusaidiana na kushirikiana wakati wa misiba, masumbuko n.k. ili kustawisha jamii zetu.
Mwl. Nyerere Wakati wa uhai wake aliwai kusema “ maadui wakubwa wa maendeleo ya kimwili na kiroho kwa bara la Afrika  ni ujinga, maradhi, umasikini na ushirikina. Ushirikina na imani za uchawi ni zaidi ya ujinga na ndio chanzo kibwa cha maradhi na  umasikini.
Katika ubatizo wale wote waliokuwa wakishiriki uchawi au uganga wanatakiwa kuwa wamejuta na kuungama matendo yote ya ushirikina waliyoshiriki, na vifaa vyao kama vitabu au hirizi viteketezwe kwa moto (Mdo 19:18-19, Efeso 5:6-12).
 Mbatizwa usijivishe ngozi ya Kondoo wakati u Mkristo itaonekana umemwahidi uongo mwana wako na kufanya mzaha mbele ya Mwenyezi Mungu.


Post a Comment