Ads (728x90)

Powered by Blogger.





“Utalii kwa wote - wote wawezeshwe” hii ni kauli mbiu ambayo kila nchi mwanachama wa shirika la Utalii Dunia (UNWTO) inaendelea kutumia hadi hapo itakapotolewa nyingine itakayoanza kutumika  Septemba mwaka huu na Tanzania ni moja ya nchi yenye vivutio vingi vya utalii duniani na ipo katika orodha ya nchi zilizopo katika umoja huo.

Tanzania tumebarikiwa kuwa na vivutio vya asili (god given) pamoja na vile vya kuanzishwa (Man made) ambavyo vinaingiza fedha nyingi za kigeni toka kwa watalii wanaotembelea hapa nchini toka kila pembe ya dunia. Hatuna budi kumwomba Mungu mara nyingi kadiri tuwezavyo kwa kutupatia raslimali hadhimu ambazo ni hazina kubwa katika sekta ya Utalii na zenye tija kwa vizazi vijavyo.

“Lugari Zoo” iliyopo katika Kijiji cha Tugutu  wilayani Mbinga, Mkoani Ruvuma ni moja ya kivutio cha Utalii cha Kutengenezwa kilichoanzishwa na Mwanajeshi Mstaafu Samweli Ndomba, baada ya yeye kutambua umuhimu wa utalii kwa watanzania na mapenzi yake toka moyoni katika Sekta ya Utalii duniani.

Lugari zoo yenye takribani hekta 127, ilianzishwa mwaka 2013 na  hadi kufikia hivi sasa ina umri wa miaka minne. Watalii wengi toka maeneo tofauti ambao wanatembelea Lugari Zoo wanapata fursa hadhimu ya kuona Ndege wa aina mbalimbali kama Tausi, Peakoc,vecharine, Kuku, Bata, njiwa aina tofauti na wengine wengi wakiwemo ndege ambao asili yao ni Mbinga.

Lakini wapo pia Wanyama wanaokula majani pamoja na wale walao nyama, kati yao pia wapo wanyama wakali na wanyama wapole. Wanyama wakali wamewekwa kwenye vibanda vya chuma kwaajili ya usalama huku wale ambao sio wakali wapo kwenye wigo wa kawaida. yapo makundi ya wanyama tofauti tofauti toka nchi mbali mbali kama vile Chui, Simba, Swala, Ngamia, Pundamilia, Fisi n.k.

 Aidha Mandhari mazuri yaliyopambwa na bustani za maua, picha zuri bila kusahau mabwawa yenye Samaki n.k, vinatoa chagizo kwa watalii wanaotembelea Lugari Zoo kwenda mara nyingi kadiri wawezavyo na wakati mwingine baadhi ya watalii wakienda Lugari Zoo hawatamani kurudi makwao. Neno “Zoo” maana yake ni bustani ya wanyama.

Katika ziara ya kiutalii iliyofanyika hivi karibuni huko Lugari Zoo na baadhi ya wafanyakazi wa Abasia ya Peramiho (Prokura) kwa lengo la kupumzisha hakiri mwanzoni mwa mwaka 2017, Msimamizi mkuu wa Kampuni hiyo Samwel Samwel Ndomba ambaye amerithi jina la Baba yake Mzee Samwel alifafanua yafuatayo kuhusu Lugari zoo:

“Asili ya jina Lugari zoo limetokana na jina la kijiji alichotokea Mmiriki  Mzee Ndomba ambaye ni Baba yangu mzazi, lengo la kutumia jina hilo ni kuenzi kijiji alichotokea pamoja na kukuza jina la kijiji chake ”
“Kabla ya yeye kustaafu kazi ya jeshi nakumbuka aliniambia kuwa kutokana na mapenzi yake katika Sekta ya Utalii Duniani lazima angeanzisha kitu chochote kinachohusiana na mambo ya utalii ambapo baada ya kustaafu ameamua kutekeleza kwa vitendo kwa kuanzisha Lugari Zoo ikiwa ni fahari kwake pia kwa wanaruvuma”

“Lugari Zoo tuna makundi ya aina tofauti tofauti ya wanyama pamoja na ndege toka maeneo tofauti duniani, kwa waliobahatika kutembelea hapa bila shaka ni mashahidi wa hilo, toka tulipoanzisha hadi kufiki hivi sasa watu kutoka sehemu tofauti wamepata fursa ya kutembea hapa Lugari Zoo, wakiwemo wale wa nje ya Tanzania” anasimulia Samweli Ndomba kisha anaendelea.

Malengo ya Lugari Zoo

“ Tofauti na kujiingizia kipato, Lugari Zoo tunaiboresha kila mwaka ili kuifanya iwe ya kimataifa kwa lengo la kutoa huduma bora kwa watu wote, binadamu wanaitaji muda wa kupumzika na kuburudika baada ya kufanya kazi kwa muda mrefu, maeneo ya kitalii kama Lugari Zoo  ni sehemu moja wapo ya kupumzika”

Wakazi wa mbinga

“ Ni mara chache kwa nabii kukubarika nyumbani kwa kuwa watu wengi wanaokuja hapa ni wageni kuliko wenyeji, inawezekana bado hawana elimu ya kutosha kuhusu maana ya utalii na hawajui faida ya kupumzisha hakiri. Uwezi kuamini kuna watu wanakaa wilayani Mbinga lakini hawajui kinachoendelea hapa ndani, nawakaribisha wakazi wote wa Mbinga pamoja na maeneo yote ya Tanzania hapa Lugari Zoo, waje wajione wenyewe mazuri ya hapa”

Chakula cha wanyama

“Wanyama wanaitaji chakula bora na kingi ili waweze kuishi, wastani kwa siku tunatumia laki mbili na kidogo kwaajili ya chakula cha ndege na wanyama, pia ili kupunguza gharama tunalazimika kuchanganya nyama na dona kwa wanyama kama jamii ya fisi na kuwafanya waendane na mazingara yetu tofauti na mazingira ya polini ya kula nyama tu (kwa kuzingatia maelekezo ya daktari wetu wa mifugo), Wanyama kama Chui anakula kilo nane (8)  za nyama  kwa siku ambapo kwa wiki anakula mara nne (4) 8*4*7000=Tshs.224000/= hiyo ni gharama ya chakula cha Chui kwa wiki”

Changamoto

“Daktari akimwacha mgonjwa katika hali zuri, baada ya muda mfupi akamkumta amefariki lazima imuume, hata kwa upande wetu tunapambana na tatizo la vifo vya wanyama hasa vile vya ghafla tunaumia sana tukikuta Sungura au Mamba amepoteza maisha. Tuna madaktari wa mifugo ambao wanawafanyia uchunguzi mara kwa mara kwaajili ya usalama wao”

“Siku zingine watalii wanaweza wakapungua na siku zingine wanakuwa wengi na ili kujihakikishia kupata watalii wengi kila siku tunaendelea kuboresha hudama zetu mara kwa mara ili kuendana na wakati tulionao”
Usalama
“Ulinzi ni mkubwa mno kwa usalama wa wanyama na kwa Raia wanaokuja na wanaoishi karibu na Lugari Zoo, tuna walinzi watano wenye silaha na mabanda ya wanyama ni imara hasa yale ya wanyama wakali kama Simba, chui n.k. vile vile tunaendelea kuimarisha kutokana na mahitaji na wakati” anafafanua Samwel Ndomba Mtoto wa Mzee Ndomba Mmiriki wa Lugari Zoo.

Kuwaongoza watalii ni moja ya kazi ngumu inayoitaji umakini mkubwa kwa kuwa watalii wengi ni watu wa aina tofauti, wapo waliosoma, wasiosoma, walevi, watoto, viziwi, wazee na hata wadadisi hasa wale wanaojifanya wanajua vitu ambavyo hawavijui, hizo ni moja ya changamoto ambazo wanakabiliana nayo wafanyakazi wa Lugari Zoo.

“Kuwaudumia wanyama na kuwaelekeza watalii inaitajika taaluma ya hali ya juu kwa kuwa wanakuja watu wa aina tofauti na wenye uelewa tofauti wa vitu. Lakini tunapata sana shida kwa wale ambao wanakuja ili kutupima au kutuchezea hakiri lakini kwa kuwa tuna mafunzo bora na uzoefu wa kutosha, kila mmoja anapata kile anachokiitaji kwa usahihi” anafafanua kiongozi wa watalii wa Lugari Zoo Richard Kawanga.

Dunia kote idadi ya watu wanaosafiri nje ya nchi yao kwa ajili ya utalii iliongezeka kwa asilimia 4.4 mwaka 2015 na hivyo kuvunja rikodi mpya kwa mwaka wa sita mfululizo.

Shirika la Umoja wa Mataifa la Utalii UNWTO lilisema kwenye taarifa yake kuwa idadi ya watalii ilifikia bilioni 1.2 mwaka 2015 na ongezeko hilo limechangia pakubwa katika ukuaji wa uchumi na uzalishaji wa ajira kwenye maeneo mengi ya dunia, kuna matarajio makubwa ya ongezeko la watalii hasa barani Asia na Pasifiki huku watalii wengi wanatarajiwa kutokea katika nchi za China, Marekani na Uingereza.

Matarajio kwa Afrika na Mashariki ya Kati hayako thabiti kwa sababu ya vitisho vya usalama na ukosefu wa takwimu sahihi kuhusu usimamizi wa vivutio vya utalii vilivyopo pamoja na idadi ya vivutio vyote kwa kila nchi usika.

Bustani ya wanyama ya Lugari ipo kwenye orodha ya vivutio vya kitalii ambavyo vinakuza kipato cha serikali ya Tanzania ambapo kutokana na amani, utulivu pia usalama uliopo Tanzania Serikali inatakiwa kuwa makini zaidi katika sekta ya utalii kupitia sera ya uwekezaji ili kuvuna fedha nyingi zaidi kupitia utalii. Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Lugari Zoo, Amina

   


Post a Comment