Ads (728x90)

Powered by Blogger.



Kwa asili Wangoni ni kabila linalotokana na ukoo wa akina Zulu na wale wa aina ya  Wathonga ambao ni kundi shiriki la kabila la Wangoni ndio walioruhusiwa kushika madaraka ya uongozi katika serikali ya kikabila.

Lakini hali hiyo ilibadilika baada ya Wangoni kupata makazi ya kudumu. Wangoni kutoka kundi la Wakatanga, Wasenga, Wasukuma n.k. waliruhusiwa kutawala kama Manduna (subchiefs) katika maeneo yao, vyeo ambavyo walikabidhiwa watu wenye akili ya kuongoza jeshi kwenye vita. Lakini amkio kuu la “Bayete” lilitumika kwa chifu Mkuu yaani Nkosi tu!


Walichofanywa Wangoni na Waingereza

Kutoka mahali ambapo Wangoni waliweka masikani yao ya kudumu, walikuwa na tabia ya kuwashambulia majirani zao. Kadiri  walivyoendelea kuviteka vijiji, makabila mengi yalijisalimisha kwa Wangoni hali iliyopelekea kabila hilo kupanuka kwa kuwa mateka wengi waliingizwa moja kwa moja kwenye kabila lao.

Lakini vijiji vingi vya wenyeji vilijisalimisha  chini ya himaya ya Wazungu (Waingereza) hivyo iliwawia vigumu sana Wangoni kuviteka na kupata matatizo walipojaribu kuviteka. Kwani waingereza ukianzia  huko Zomba Nyasaland (Malawi) chini ya Afisa wa Kiingereza aliyejulikana kwa jina  la Sharpe aliliongoza jeshi la kiingereza ambalo lilijitoa mhanga  dhidi ya  Wangoni kisha akafanya nao vita  kwa lengo la kuwazuia Wangoni wasiwashambulie watu (wenyeji) waliokuwa chini yao. Wangoni aina  ya Ngomani  walishambuliwa na kikosi hicho cha jeshi la Waingereza na hivi kulazimika kusalimu amri na kukubali kuwa chini ya uingereza. Waliojisalimisha kwa waingereza bila kumwaga damu, walikuwa ni Wangoni wa aina ya  Mbelwa.

Mwaka 1889 Afisa wa Kiingereza ililichukua jeshi la Wangoni wa aina ya Mpezeni na kuliweka chini ya utawala wa Waingereza. Lakini Afisa huyo alipokwenda likizo (Ulaya). Jeshi la Mpezeni liliamua kuasi chini ya Mpezeni mwenyewe na mwanae aliyefahamika kwa jina la Nsingu  kisha wakakataa kabisa kutawaliwa na Waingereza ambapo waliamua kuanzisha vita dhidi ya wazungu kwa kuwafuata hadi Forte Jameson sehemu iliyokaliwa na waingereza wengi sana.

Mkuu wa kikosi cha Waingereza Bw. Brake, aliyewalisi kutoka  “Bua ili kuliimalisha jeshi la waingereza na kulipiga jeki, alifaulu kulishinda jeshi la Wangoni wa Mpezeni. Mzungu huyo kwa ushenzi alimwua Nsingu mwana wa Mpezeni.  Mpezeni mwenyewe walimfanyia unyama wa kumchomea  mashamba yake ya chakula katika vijiji vyake na baadaye Wazungu  wakateka mifugo yake yote. Mpezeni baada ya kukiona kisanga hicho  yeye na raia wake waliamua kujisalimisha kwa waiingereza. 

Mambo hayo yote yalitendeka mwaka 1897. Mpenzeni alikufa mwaka 1900 na kiti chake kikatwaliwa na Mpezeni Cholowa, Mtwalo alikufa mwaka 1890, Mbelwa alikufa mwaka 1891 mrithi wake alikuwa Chimtungu aliyekufa mwaka 1924. Mrithi wa Chimtungu alikuwa Mkuzo  aliyekufa mwaka 1927, na kurithiwa na Lazaro Chikupizga.

Wangoni wa Afrika ya Kati
Hadi leo bado kuna makundi matatu ya Wangoni waishio Afrika ya Kati ambayo ni Wangoni wa aina ya Mpezeni, Mbelwa na Mseko. Kwa kuingiliana katika suala la kuoana na makabila ya wenyeji, Wangoni hao walipanua kabila lao na kuongeza nguvu huku makabila yaliyotawaliwa yakiingizwa kwenye kabila la Wangoni.

Hali hiyo ilipelekea idadi ya Wangoni kuongezeka toka 25% hadi 75% katika kabila la Wangoni hasa vijijini ambako kwa kiasi kukubwa kunakaliwa na  Wangoni halisi. Baadhi ya Wangoni kiidadi  ni watu wenye kuongea lugha zaidi ya moja. Mara nyingi Wangoni hao huacha kuongea lugha yao na kuongea lugha za wenyeji.

Mwaka 1936 Wangoni wa Rhodesia ya Kaskazini (Wangoni wa Mpezeni)  walikuwa 80, 000 kiidadi, wakati wale walioishi huko Nyasaland (Malawi)  walikuwa 250,000. Kama unafuatilia kwa ukaribu idadi ya kundi hilo la Wangoni huko Afrika ya Kati, ni kitambulisho na ushaidi tosha kwamba, Wangoni waliofika huku Tanganyika na kuweka makazi yao ya kudumu hususani Songea  ni sehemu ya ndogo tu ya kabila lote.

Katika Afrika ya Kati kabila la Wangoni lilijulikana kwa jina la Angoni badala ya Wangoni kwani jina Angoni ni neno la uwingi kutoka lugha ya kichewa na kinyanja. Mfano wa maneno hayo ni:
Neno  (Kinyanja  au  Kichewa)                                                   
Mtu (Umoja)  Mundu  (Uwingi) Andu, Mtoto (Umoja)  Mwana  (Uwingi) And, Msafiri (Umoja)  Mlendo (Uwingi)  Alendo
Mjumbe (Umoja) Mtenga (Uwingi) Atenga Mzungu (Umoja)  Mzungu (Uwingi) Azungu,   (Umoja)  Mngoni (Uwingi)  Angoni

Makabila yaliyounda kabila la Wangoni Afrika ya Kati

Wangoni halisi huko Afrika ya Kati wametokana na makabila mengi yaliyojichanganya  na Wangoni wenye asili ya Kizulu na Kithonga. Kama ilivyo Tanganyika kwamba Wangoni walipowasili (Tanganyika) waliyakuta makabila mengine yakiishi, lakini Wangoni waliyateka na kuyaingiza katika kabila lao.  Makabila hayo ya Afika yaliyoshiriki kuunda kabila la Kingoni ni pamoja na Waswazi, Wathonga, Wakalanga, Wasenga pamoja na Wasukuma kwa mujibu wa mwandishi  aitwaye Cullen Young. Ukoo wa Angoni huko Afrika ya Kati una makundi yafuatayo:

(a)          Wenye Asili ya Kiswazi: akina Chiziwa, Chongwe, Daba, Gama, Gausi, Jere, Kambuli, Mabaso, Mdhlopa, Madisi, Mafuleka, Mbuyisela, Ndhluli, Mgawezulu, Mhlanga, Mkala, Mkaripi, Mlota, Mvalo, Molabandaba, Nhlane, Nkosi, Nyumayo, Nyambosi, Pakati, Quangwane, Sibande, Sichi, Tawi na Tole.

(b)          Majina ya ukoo yenye asili ya Wakalanga ni akina  Chibambo, Gumbo, Hara, Mapara, Mbizi, Mloyo, Nali, Ndoro, Neba, Nungu, Nyanguru, shaba, shumba, Soko na Ziba.

(c)           Majina  ya ukoo yenye asili ya Wasenga ni akina Lungu, Miti, Mumba, Mvula, Mwanza, Ng’oma, Nguruwe na Tembo.

(d)          Majina ya ukoo yenye asili ya Wasukuma ni akina Chipeta, Chisi, Chuku, Mchizi, Mkawe, Mlenje, Mpepo, Msmziya, Nkana, Ntara, Nyika, Nyoni na Tindi.

Majina ya ukoo kama akina Chongwe, Gama, Nkosi, Nyumayo, Tole, Nkuna, Hara, Mapara, Moyo, Soko, n.k ni majina ya ukoo ya Wangoni kwa hapa Tanganyika. Kadiri ya orodha hii ya majina ya ukoo wa kabila la Wangoni yamo majina hayo hata kwa Wangoni wanaoishi huko Afrika ya Kati. Hata hivyo ifahamike kwamba si watu wote wa aina hiyo wenye majina hayo ya ukoo wana uhusiano na kabila la Kizulu, na pengine waliingia humo bila kuwa Wangoni wa Kizulu.


Post a Comment