Ads (728x90)

Powered by Blogger.




Image result for wamatengo
Na Alex Mapunda
Wamatengo ni  kabila dogo linalopatikana mkoani Ruvuma katika wilaya ya Mbinga upande wa Mashariki, Wamatengo wanaishi sehemu za milimani eneo ambalo lina hali zuri ya hewa pamoja na ardhi yenye rutuba inayowawezesha kulima mazao kama kahawa, mahindi, ngano n.k. kama ilivyo kwa makabila mengine Wamatengo nao wanasifa ya ukarimu, kuchapaka kazi na hata katika upande wa mahusiano wana vitu vingi vinavyowatofautisha na makabila mengine.

Katika suala la mahusiano  Kijana wa kiume anapobalehe wazazi humshawishi atafute mwenza kwa kumwambia; “sasa tafuta jiko lako, wewe sasa ni mkubwa kwa kuoa”. Miaka ya nyuma ilikuwa sio rahisi kumpata mchumba kwa sababu wasichana hawakuruhusiwa kwenda shule wala kukusanyika katika matamasha kama ilivyo sasa. Vijana wa kiume walilazimika kwenda kuwinda wasichana kwenye shughuli za matanga, michezo ya ngoma maarufu kwa jina la Mhambo, Chihoda au kwenda nyumbani kwa wazazi wake.

Kwa kawaida Ndoa ni muungano wa hiari kati ya mume na mke wenye nia ya kuishi pamoja mpaka mwisho wa maisha yao au mmoja wao, ili ndoa iweze kufungwa sheria inafafanua kuwa umri wa wanandoa uanzie miaka 18 na kuendelea, licha ya kwamba vijana wanaweza wakaoana chini ya umri huo kwa sababu maalamu (chini ya uangalizi wa wazazi) kwa kibari cha mahakama. Kuna ndoa ya Kidini, Serikali pamoja na Kimila.

Asilimia kubwa, Wamatengo wanafunga ndoa za kimila kuliko ndoa za kidini au za serikali na wanaishi uchumba bila kufunga ndoa ya Kanisani kwa muda mrefu wakati wao ni wakristo, sheria za Kanisa haziruhusu wakristo wa jinsia tofauti kuishi pamoja kama bibi na bwana bila kufunga ndoa. Amri ya 06 kati ya Amri 10 za Mungu inafafanua suala la unzizi; kufanya mapenzi bila kufunga ndoa ni dhambi kwa mujibu wa Kanisa. Baadhi ya sababu zinazowafanya wamatendo waishi uchumba muda mrefu bila kufunga ndoa:

Utandawazi; Hadi kufikia miaka ya 1990 taratibu za Kanisa kuhusu ndoa pamoja na taratibu za kimala zilifanana kwa kiasi kikubwa; moja wapo ni kuto waruhusu wachumba kuishi pamoja bila kufunga ndoa au bila kutoa mahari na kipindi kile wamisionari walifanikiwa kulifikisha neno la Mungu kwa usahihi mikononi mwa  wazee wa kimatengo hivyo iilikuwa rahisi kuwashawishi vijana wao kufunga ndoa kabla ya kuishi  pamoja. Kwa sasa utandawazi umeingilia kati vijana wanakutana tu njiani na kwenda kuishi pamoja bila wazazi kupewa taarifa wala hawajali amri 10 za mwenyenzi Mungu. Hivyo ni mara chache mno kushuhudia vijana wakifunga ndoa kabla ya kuanza kuishi pamoja.

Tamaa; Wanaume wengi wa Kimatengo wana tamaa ya kuoa mwanamke zaidi ya mmoja au baada ya kuoana anaishi nae kwa muda fulani tu! na kuoa mwingine, hivyo wanaogopa wakifunga ndoa watabanwa na sheria pindi watakapoamua kumwacha wa kwanza na kuoa mwingine: “wengi ni wajanja wanaishi na mwanamke kijanja wakimchoka wanatafuta mwingine au anaweza akaoa mke wa pili na kumwambia yule wa kwanza kwamba naenda kufunga ndoa na huyu wa pili” anasimulia Mzee Union Komba Mkazi wa kijiji cha Manzeye Wilayani Mbinga. Wanaume wa kimatengo hawajazoea kuishi na mwamke mmoja toka ujana hadi uzee hali ambayo inawafanya waoe mke zaidi ya Mmoja maarufu kwa jina la “Mitara” 

Mahari; Baadhi ya wazazi wanaweka kipingamizi cha kufunga ndoa kwa kigezo cha mahari, kabla ya harusi wanataka upande wa mwanaume watoe kwanza mahari yote waliyokubaliana tofauti huweka zuio na wakilazimisha kufunga hutoa laana kwa binti yao kwa kusema “kama tulikuzaa sisi basi kuanzia leo sisi sio wazazi wako tena, na tusikuone kwetu”. Licha ya kwamba siku hizi wazazi wengi wameelimika na suala la kuwazuia vijana wasifunge ndoa kwa sababu ya mahari  limepungua kwa kiasi kikubwa mno.

Elimu; “Baadhi ya vijana wanapoenda masomoni wana kawaida ya kuoa na kumwacha mwanamke kwa wazazi wao bila kufunga ndoa, suala ambalo ni kinyume na sheria za Kanisa ambapo hadi kumaliza masomo inachukua muda mrefu, hali hii inapelekea wao kuishi katika uchumba kwa muda mrefu bila kufunga ndoa kwa miaka 10 hadi 35” alisema Mzee Komba.

Viongozi wa dini wana kazi kubwa sana ya kuwaelimisha Wamatengo ili waweze kufunga ndoa kabla ya kuishi pamoja kwa kuwa hadi sasa wamejitahidi kutoa elimu lakini hakuna mafanikio. Utandawazi umeingilia kati na vijana hawashikiki wala hawaambiliki, wengi wao utasikia wakisema “suala la kufunga ndoa kabla ya tendo ni sawa na kuuziana mbuzi kwenye gunia” na sheria za Kanisa haziruhusu kufanya mapenzi bila kufunga ndoa kwa (Wakristo).

Wazazi; Wazazi ni kikwazo kikubwa mno kwa vijana wa kimatengo katika suala la kufunga ndoa, wao ndio washauri wakuu na wanauwezo wa kusema ndoa ifungwe au isifungwe. Wazazi wanaamini kwamba kipimo kimojawapo cha vijana wao kuishi pamoja bila kuachana (milele) ni lazima waishi kwanza bila ndoa angalau miaka mitano (05), hata kwa vijana waliosoma nao wameshindwa kutumia taalama zao ili kuwashawishi wanaoshikilia mfumo huo waachane nao; cha kushangaza  na wao wametumbukia shimoni na kusahau taratibu na maadili ya Kanisa Katoliki.

Sifa; Kwenye suala la Ndoa Wamatengo wengi wanapenda kuonekana, kijana anatumia miaka 15 ili kujiandaa na harusi kwa kuamini kwamba ndoa bila sherehe inapoteza thamani, hata kama kipato cha wanandoa ni kidogo wanajitahidi kwa namana yeyote ile ili kufanikisha sherehe. Ndoa zinazofungwa bila sherehe zinaitwa ndio za “Mafungu” au “Ndio za mikeka” au “Ndoa za walalahoi” na mara nyingi wanandoa wanaofunga ndoa ya mkeka wanakosa furaha au amani  kwa kuwa wanachekwa na wenzao katika matukio mbali mbali kama vile sherehe, misiba n.k.

Kuiga; “Kwa kuwa Baba alifunga ndoa baada ya kuishi uchumba kwa kipindi cha miaka 20 basi na mimi nitakaa kama Baba au rafiki yangu alifanya sherehe kubwa siku ya arusi yake basi na mimi nitafanya sherehe kubwa kama yeye, pasipo kuangalia hali ya uchumi wangu ipoje zoezi ambalo linapelekea wanandoa kujiingiza kwenye madeni yasiyo ya lazima” anaeleza Damas Januari kijana wa kimatengo ambaye toka ameoa ana miaka minne na bado hayafunga ndoa.

Miaka 25 ambayo Katekista Jonas Komba amefanya kazi ya uchungaji katika Kanisa la Manzeye huko Mbinga, ndoa alizoandikisha kwa kutumia mkono wake wa kulia, zote wahusika waliishi pamoja (uchumba) kwa kipindi kisichopungua miaka mitano na zaidi; “wengi wanaoana bila kufuata taratibu za Kanisa, kwa madai kwamba wanaenda kuchunguzana tabia, mara nyingi wanahukumiwa na mafundisho ya Komunio ya kwanza au kipaimara kwa watoto wao, wasiofunga ndoa tunawasitishia huduma za Kanisa. Kufunga ndoa ni tendo la kheri, anayejua kuhusu hatima ya maisha yetu ya hapa duniani ni Mungu peke yake” alilisitiza Kat. Komba.

Padre Christian Mhagama amefanya wa Jimbo Katoliki la Mbinga, hivi karibuni aliliambia Gazeti la Mwenge kwamba ndoa ambazo amefungisha zinazowahusu Wamatengo hadi kufikia leo ni zile tu! ambazo wanandoa waliishi katika hali ya uchumba kuanzia miaka Saba (07) na kuendelea; “ Wamatengo wanafunga ndoa baada ya kuishi pamoja kwa muda mrefu, kitu ambacho kinatushangaza wengi. Wanafunga ndoa baada ya kuishi miaka 10  hadi 20. Kila nikipata fursa ya kufungisha ndoa, kwanza nataja Kanisani idadi ya miaka ambayo Bibi na Bwana harusi wameishi katika hali ya uchumba, ikiwa chini ya miaka 10 basi tunawapongeza kwa kufunga ndoa mapema” alisema Padre Mhagama (yupo mbinga kwa takribani miaka 11 sasa).

Yatupasa kutafakari kwa kina kuhusu namna ambavyo tutaenda mbinguni bila kuchoka, suala la Wakristo kuishi uchumba bila kufunga ndoa lipo katika makabila mengi na sio kwa Wamatengo tu! Sote inatupasa kutubu zambi zetu, kumrudia Mwenyenzi Mungu na kushika amri zake, Amina.



Post a Comment