Ads (728x90)

Powered by Blogger.





Na Alex Mapunda, Ruvuma

TIMU ya Parangu Fc imeendelea kugawa pointi kwa wapinzani wake katika mashindano ya Ansgar Cup ngazi ya Tarafa, mara baada ya kukumbana na kipigo cha bao 4-1 dhidi ya Kilagano Fc kwenye dimba la Ansigar Peramiho.


Katika mchezo huo ambao Parangu ilielemewa kila idara, mabao ya Kilagano Fc yalifungwa na Liambi Kipanga dakika ya 26, Fred Membe dakika ya 31, Frey Ngonyani dakika ya 34 kabla  Jofrey Soka kushindilia msumari wa nne kwenye geneza la Parangu mnamo dakika 78. Bao la kufutia machozi kwa upande wa Parangu Fc liliwekwa kimiani na Erick Nyoni dakika ya 62 katika ungwe ya lala salama (Kipindi ya pili). 

Kivutio kikubwa katika mchezo huo ni kwamba wachezaji wote ambao walivaa jezi namba 11, yaani Frey Ngonyani toka Kilagano Fc pamoja na Godfrey Hala toka Parangu Fc walitolewa nje kwa kadi nyekungu baada ya kukiuka sheria na taratibu za mpira wa miguu. 

Timu zote mbili zilikumbana na kichapo katika michezo yake ya awali ambapo timu ya Parangu ilitandikwa bao 2-1 dhidi ya timu ya Litisha wakati Kilagano Fc ilikung’utwa na Peramiho (Afya Fc) kwa jumla ya bao 3-0.

Katika michezo mingine timu toka kata ya Litisha iliifunga Peramiho (Afya Fc) bao 1-0, Liganga Fc iliichabanga Mpandangindo bao 3-2 kisha Maposeni Fc ikaishindilia Lilambo bao 2-1 katika mchezo ambao Lilambo waliianzisha vurugu.
 
Mwaka huu zawadi zimeboreshwa toka shilingi 300,000/= kwa washindi wa kwanza hadi shilingi 400,000/=, 250,000/= washindi wa pili hadi shilingi 300,000 pamoja na 150,000/= washindi wa tatu hadi 200,000/= huku mchezaji bora akiambulia kifuta jasho cha shilingi 50,000/=  hali ambayo imesababisha ongezeko la ushindani na kila timu shiriki inatamani kunyakua ubingwa wa mshindano hayo.

Ansgar cup ni moja ya ligi kongwe mkoani Ruvuma na imedumu kwa zaidi ya miaka 20, lengo kubwa la mashindano ya Ansgar yanayoandaliwa na mkurugenzi wa Hospitali ya Peramiho Dkt Ansigar Stuffe OSB ni kuibua vipaji kwa wachezaji, burudani baada ya kazi, kuongeza soko la biashara kwa wafanyabiashara wa tarafa ya Peramiho n.k. 

Baadhi ya wachezaji waliotokea Ansgar Cup ni pamoja Pato Ngonyani (Maji Maji, na Yanga), Anold Nguruchi na wengine wengi.




Post a Comment