Ads (728x90)

Powered by Blogger.


Na Albano Midelo


Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Songea yalianza kutolewa mwaka 1984  kwa kutumia majengo yaliokuwepo katika viwanja vya Sabasaba vilivyopo Matarawe Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma.

Katika kipindi hicho chuo kilikuwa na uwezo  wa kutoa mafunzo kwa wanafunzi 60 tu katika fani tatu ambazo ni ufundi magari, ujenzi na useremala.

Mkuu wa Chuo cha Elimu na Mafunzo ya Ufundi Stadi VETA Songea Gideon Ole Lairumbe anasema ujenzi wa majengo ya kudumu ya chuo hicho katika eneo la Msamala Manispaa ya Songea ulianza mwaka 2003 na kukamilika mwaka 2005.
Lairumbe anabainisha kuwa ujenzi huo ulijumuisha karakana tisa za mafunzo, jengo la utawala, maktaba, madarasa, jengo la maliwato, uzio na chumba cha mitambo ya umeme.

Anabainisha kuwa katika ujenzi huo zaidi ya sh.bilioni 1.654 zilitumika kati ya fedha hizo, ujenzi wa majengo zilitumika zaidi ya sh.milioni 975, Mshauri elekezi zaidi ya sh.milioni 86.45 na ununuzi wa mitambo na vifaa vya mafunzo zilitumika zaidi ya sh.milioni 592.

Anasema baada ya ujenzi wa chuo hicho kukamilika, uwezo wa kudahili wanafunzi katika chuo umeongezeka toka wanafunzi 60 hadi 250 kwa mwaka.

Hata hivyo Mkuu huyo wa chuo anabainisha kuwa  hadi kufikia mwaka 2017 chuo hicho kina wanachuo 646 kati yao wanachuo wanaosomea hatua ya kwanza (level one) wanaume 253 na wanawake 88, wanaosomea hatua ya pili wanaume ni 176 na wanawake 67 na wanaosomea hatua ya tatu wanaume ni 55 na wanawake saba.

“Chuo kinatoa mafunzo ya muda mrefu na muda mfupi, kwa kozi za muda mrefu mafunzo yanayotolewa ni katika fani za ufundi magari, uungaji vyuma, umeme wa magari, umeme wa majumba, useremala, uashi, ufundi bomba, ushonaji na uhazili na kompyta’’, anasema Lairumbe.

Kwa mujibu wa Mkuu huyo hadi sasa wanafunzi ambao wanaendelea na mafunzo ya muda mrefu ni 591 na kwamba chuo hicho bado kinaendelea kupokea wanafunzi wa mwaka wa kwanza na kwamba mafunzo yanatolewa katika awamu mbili tofauti asubuhi na mchana.

Mkuu huyo wa Chuo anayataja mafunzo ya muda mfupi  yanayotolewa na VETA Songea kuwa ni fani za udereva wa magari daraja D, udereva wa magari ya abiria na uhazili.

Fani nyingine ni ukarabati wa kompyuta, utumiaji wa kompyuta, umeme wa majumba, umeme wa jua, ulimbwende(cosmetology), utengenezaji wa dawa za usafi, sabuni za maji, upishi na utengenezaji wa batiki na ujasirimali.

Takwimu zinaonesha kuwa tangu kuanzishwa kwa chuo hicho hadi kufikia mwaka 2016 wahitimu wa mafunzo ya muda mfupi ni 3013 kati yao wasichana 523 na wavulana 2490.

Miongoni mwa walionufaika na VETA Songea ni wahitimu wa kwanza 20 wa fani ya ushonaji ambao walikabidhiwa vifaa vya ushonaji  vyenye thamani ya sh.milioni 10  kwa ajili ya kuwajengea uwezo wahitimu wa fani ya ushonaji kabla ya  hawajaingia rasmi kwenye soko la ajira.

“Chuo kiliamua kuanza na fani ya ushonaji kuwapa motisha ya vifaa kutokana na uzoefu kuonesha kuwa wanaojiunga na fani hii wengi ni wanafunzi wa kike ambao pi waathirika zaidi wa ukosefu wa ajira  nchini’’, anasema Mkuu wa Chuo.
Anasema kuwa chuo hicho kimefanikiwa kupata jengo jipya ambalo linajumuisha maabara za Teknolojia ya Habari na Mawasiliano(TEHAMA), madarasa na ofisi za walimu.

Sanjari na ufundishaji wa kozi fupi, Mkuu huyo wa chuo anasema chuo kinafundisha kozi fupi za udereva wa pikipiki, udereva wa magari, utengenezaji wa  sabuni na batiki na kwamba lengo ni kuwafikia wahitaji wote mahali walipo ili kupunguza changamoto ya ajira.

Licha ya kutoa kozi hizo katika Manispaa ya Songea mkoani Ruvuma, Mkuu wa Chuo hicho anasema, VETA Songea pia imefanikiwa kufundisha kozi hizo katika wilaya za Njombe, Ludewa na Makete mkoani Njombe.


“Chuo pia kinatoa mafunzo kwa kushirikiana na viwanda na maeneo mbalimbali ya kazi, lengo likiwa ni kuwajengea uwezo zaidi wafanyakazi viwandani ili kuongeza tija’’, anasema Lairumbe.

Anasema VETA Songea inashirikiana na viwanda na kampuni mbalimbali zikiwemo UNILEVER ambayo ni kampuni ya kiwanda cha chai, Kampuni ya MANTRA ya mgodi wa uranium na kampuni ya Food Security ambayo wafanyakazi wake 31 wamepata mafunzo ya muda mfupi kupitia VETA.
Anayataja matarajio ya chuo hicho kuwa ni kuanzisha fani ya uandaaji wa vyakula (Food Production), utengenezaji wa vifaa vya kilimo(Agro Mechanics) na kozi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano(TEHAMA).

Anatoa rai kwa serikali na wadau wengine kuiangalia VETA kama mkombozi wa ajira kwa vijana hasa katika kipindi hiki ambacho Tanzania na Dunia nzima inakabiliwa na janga la ukosefu wa ajira ambapo vijana ndiyo waathirika wakuu.

Waziri Mkuu Mstaafu Mizengo Pinda wakati anafungua chuo cha VETA Songea mwaka 2013, pamoja na mambo mengine aliagiza Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi kusaidia kuongeza nafasi za mafunzo katika vyuo vya VETA ili vijana wengi wanaomaliza shule za msingi na sekondari waweze kupata nafasi ya kujifunza kozi mbalimbali ambazo zitawawezesha kuajiriwa na kujiajiri.

Naibu Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhandisi Stella Manyanya anasema kwa kutambua umuhimu wa elimu ya mafunzo ya ufundi stadi, serikali inaendelea kujenga vyuo vipya vya VETA katika mikoa na wilaya mbalimbali nchini.

Mhandisi Manyanya anasisitiza kuwa serikali itaendelea kusimamia mafunzo ya ufundi stadi nchini kama yalivyoelekezwa katika sera ili kusaidia kukuza uchumi kupitia mafunzo ya VETA huku uhamasishaji zaidi ukiwekwa katika ubunifu na ujasiriamali.



Post a Comment