Ads (728x90)

Powered by Blogger.



 
Watu wa Mataifa mbalimbali hapa ulimwenguni wana mitazamo tofauti kuhusu hali ya mwanadamu baada ya kifo “nchi ya wafu”. wenyeji wa Amerika (Red Indians) waliamini kwamba baada ya kifo chake mtu uingia mahali pazuri pa kawaida.

Lakini baadhi ya Waskandinavia wa zamani walifikiri kuwa nchi ya wafu kama mahali pa milo mikubwa mikubwa na heri kwa jumla. Watu wa mashariki ya kati pia walikuwa na wazo lao kuhusu peponi.

Tena uislamu una mafundisho yake juu ya “Jaha” na ‘Jehanum”. Waafrika pia toka zamani wana mawazo mbali mbali kuhusu “kuzimu” na hali ya wale waliokufa.

Katika makala haya tutazame habari za wafu kiujumla kama linavyofundisha Kanisa Katoliki upande wa ukristo wetu. Mafundisho hayo yatatusaidia  kuimarisha imani yetu, kuondoa hofu juu ya kifo na kupenda kufa katika hali njema na baadaye kuishi na Mungu huko mbinguni milele yote.

Mahali walipo wafu kadiri ya maandiko matakatifu



Katika imani ya Kristo na mafundisho ya Kanisa Katoliki, ufufuko na hukumu ya mwisho zitatangulia maisha ya milele.

Swali katika makala haya ni wafu wako wapi baada ya kifo na kabla ya kiyama? Kwa sababu maalum Agano la Kale halivutwi na swali la maisha ya baadaye. Hivyo tutachunguza jibu la swali letu hasa katika Agano Jipya.

Ingawa Agano Jipya halielezi habari hizi kwa uwazi, ila limetoa dokezo kadhaa. zaidi lakaza habari za kiyama, hukumu ya mwisho na uzima wa milele.  Hata hivyo tujaribu kuchunguza swali hili kwa msaada wa dokezo hizo  tunazozipata katika Agano Jipya.

Inawezekana ya kwamba msomaji baada ya kusoma kifungu hiki atasema  “maelezo haya ni kufikirifikiri tu” Tunamkaribisha msomaji wa namna hii atoe maelezo yake yeye mwenyewe.

Hapa tena lazima tuache mlango wazi kwa tafsiri na mikazo mbalimbali kwa kila hali, swali letu la kifungu hiki ndilo muhimu sana katika mazingira ya kiafrika na kwa mwanadamu yeyote kwa jumla.

Agano Jipya na habari za wafu 

Mistari fulani ya Agano Jipya yasema kwamba wafu wamelala usingizini (Taz. Mt 27:52, Yoh. 11:11, Mdo 7:60, 13:36, 1 Kor 11:30, 15:6, 18, 20, 51, 1Thes 4:13-15).
Kutokana na mistari hiyo, baadhi ya wataalam wa Biblia hudai ya kwamba kifo ni kifo cha mwili na Roho pia  (K.m Poul Athaus na Emil Brunner).

Yaani hakuna sehemu yeyote ya mtu iendeleayo kuwako baada ya kifo. Baada ya kifo mtu hubaki katika ukumbuko  wa Mungu tu. na katika kiyama  Mungu atamwumba upya kwa kufuata ukumbuko wake.

Nguvu ya elezo hilo ni kwamba lapatana na maoni ya utabibu na sayansi nyingine za leo kuhusu mtu, jinsi alivyo kitu kizima.

Mtu hawezi kugawanyika katika sehemu mbali mbali. Mwili na roho haviwezi kutengana. Kwa kweli yaonekana wazi kwamba ni hivyo katika maisha yetu ya hapa duniani.

Kwa mfano magonjwa mengi ya kimwili, vidonda vya tumbo, magonjwa mbalimbali ya moyo n.k. yana  asili zao kwa upande wa roho ya mtu (Psycho- Somatic diseases).

Vile vile tukio  fulani la kimwili huweza kugusa roho ya mtu kwa mfano akigongwa kichwani vibaya na gari barabarani, akili yake yaweza kuharibika. Katika maisha roho haiwezi kutenganishwa na mwili, wala mwili kutenganishwa na roho.

Agano Jipya na suala la uwepo wa nafsi ya mtu mahali fulani

Lakini tukumbuke kwamba hapa hatushughuliki na habari za maisha wa uhai, bali ni kifo na hali ya baadaye. Kudai ya kuwa katika Agano Jipya kulala (usingizini) kwa maanisha kifo cha mwili na roho labda ni sawa.
Mtu aliyelala bado yupo au yuko, ila kwa hali nyingine  katika Agano Jipya neno kulala lilikihusu kifo hukaza habari za kufufuka kama kuamka kuliko habari za kifo cha mwili na roho.

Elezo hilo la kifo cha namna hii haliwezi kukubarika  nasi hasa kwa sababu ya dokezo za aina nyingine za Agano Jipya.

Agano Jipya hudokeza wazi ya kutosha kwamba baada ya kifo na kabla ya kiyama mtu huendelea kuwako kwa njia fulani. 

Yesu aliwaonya wanafunzi wake “msiogope wauuao mwili, wasiweze kuiua na roho (Mt 10:28). Daktari Luka akisimulia juu ya binti wa Yairo, asema: “Roho yake ikamrejea , naye mara hiyo akasimama” (Lk 8:55). Stephano alipigwa kwa mawe, aliomba na kusema: “Bwana Yesu, pokea roho yangu” (Mdo 7:59, tazama pia (Lk 23:46).

Pia tukumbuke pia juu ya Bwana wetu Yesu Kristo wakati kabla ya kufa kwake msalabani alivyomwahidi yule mhalifu wa pili aliyesulibiwa pamoja naye na kusema: “leo hivi utakuwa pamoja nami peponi (Lk 23:43).

Pia tukumbuke hapa mfano wa Yesu juu ya yule tajiri na Lazaro (Lk 16:19-31) Paulo Mtume naye kwa upande wake aliugua katika mateso mengi: “Tuna moyo mkuu, nasi tunaona ni afadhali kutokuwamo katika mwili na kukaa pamoja na Bwana” (2 Kor 5:8, Taz pia Flp 1:23).

Anasisitiza kwamba hata mauti haiwezi kutengana na upendo wa Mungu (Rum 8:38-39). Mwandishi wa waraka kwa waebrania ataja wingu kubwa la mashaidi ambalo hutuzunguka (Ebr 12:1
Na katika (1Petro 3:18-19) na 4:6 twapata habari za Yesu jinsi alivyowahubiri roho waliokaa kifungoni. Mistari hiyo ni msingi wa Biblia kwa kukiri kwa wakristo katika ibada kuhusu Kristo: “Akashuka kuzimu”.

Ufunuo 6:9-11 kwa upande wake yataja habari za roho za wale waliochinjwa kwa ajili ya neno la Mungu na ushuhuda wao.

Katika kifo mwili hufa na sehemu nyingine ya mtu hutengana nao. Twaweza kuiita sehemu hiyo kwa maneno mbalimbali: “roho”, “Nafsi” n.k. Jambo muhimu hapa sio neno fulani litumikalo. 

Jambo kuu ndilo ya kwamba kutokana na mafundisho ya Agano Jipya kwa njia fulani mtu huendelea kuwako baada ya kifo cha kimwili (kwa upande wa Agano la kale Taz dokezo la Zab 49:14-15, 73:24, 139, Mhu 12-:7, Eze 26:20, 32:17-32).
Baadhi ya watheolojia hukataa maelezo hayo kama wazo la dini nyingine ama wazo la kifilosofia. Wengine hudai kwamba maelezo hayo ni mabaki ya imani ya zamani kuhusu roho (Animism).

Lakini tusisahau ya kwamba mawazo ya fulani ya dini nyingine na Filosofia na hata maoni ya zamani ambayo watu wengine huyaita “Primitive” yaweza kuwa kweli (Taz mfano wa Mungu na ufahamu wa asili kuhusu Mungu uk. 9-13).

Wafu wapo wapi?

Mpasa sasa Biblia imetupa nuru ya kutosha lakini sasa tujaribu kujibu swali hili. Tulichunguza kwa kutokana na dokezo kadhaa tu.
Labda peponi (Lk 23:43) ama kuzimu (Lk 16:23), ni hali maalumu kuliko mahali penyewe hasa. Katika theologia kuita hali hiyo “hali ya katikati” maana yake ni hile hali ya katikati ya kifo na kufufuka.
Inaonekana katika hali hiyo ya katikati mtu huwa katika hali ya unafsi ule ule, ambao alikuwa nao duniani humu Lk 16:22-23) yaani, Paulo bado ni Paulo, yule tajiri ni mtu yule yule na Lazaro ni Lazaro.
Licha ya kutambua unafasi wake mtu awafahamu watu wengine pia (Lk 16:23) kwa njia fulani huwezi kufahamu hata maisha ya wale waishio duniani (Lk 16:22-24). Hali hizo mbili huzitangulia ufufuko kwa uzima na ufufuko kwa hukumu (Lk 16:26, Yoh 5:28-29).
Kuhusu wale wasiosikia  habari njema, Mungu labda huwapa nafasi hiyo huko kuzimu maneno ya Lk 16:26 kuhusu shimo kubwa hayapingani na uwezekano huo.
Tukisoma sura nzima ya 16 ya mwinjili Luka, twaona kwamba yule tajiri alikuwa mojawapo ya mafarisayo. Kwa hiyo bila shaka alijua mapenzi ya Mungu.
Basi ikiwa maelezo hayo ni sawa, katika kiyama ule unafsi utavikwa mwili mpya. Kwa maneno mengine utalinganishwa na mwili wa roho ama mwili wa mbinguni (1Kor 15:40,44).
 
Hitimisho

Kamati inayoshughulika na maelezo ya imani katika Kanisa Katoliki na kutoa mawaidha ambayo hutiwa sahihi na Papa kuhusu hali ya wanadamu baada ya kufa hutuelekeza mambo yafuatayo ili imani yetu iweze kudumu na kuimarika na kutembea katika mwanga juu ya imani upande wa kifo.

Mafundisho ya Kanisa Katoliki kuhusu wafu:

(A) Wakristo wanasadiki ya kuwa wafu watafufuka.

(B) Ufufuko wamhusu mtu mzima.

(C) Baada ya kifo nafsi ya kibinadamu hudumu yaani huendelea kujijua mwenyewe kama nafsi (Mimi), kuwa na dhamiri na utashi. Kwa kifupi mwanadamu aliyekufa huitwa roho (lihoka).

(D) Madhehebu ya mazishi na ibada kuhusu marehemu huwa na maana halisi wala haifai kuvipuuza.

(E) Kadiri ya maandiko matakatifu sisi wakristu tunangojea kurudi kwa Bwana katika utukufu.

(F)  Kuchukuliwa kwa Bikra Maria mbinguni humaanisha kutukuzwa kwa sisi sote.
(G) Tunasadiki ya kuwa wenye haki wanakuwa na heri pamoja na Kristo na wasio na haki walainiwa milele wasiweze kumwona Mungu.

Pia tunasadiki kwamba wenye haki waweza kusafishwa kabla ya kumtazama Mungu uso kwa uso, kwa upande mmoja sisi wakristo tunayo imani thabiti ya kuwa tutadumu kuishi ndani ya Kristo baada ya kufa.

Kwa upande mwingine twajua pia yakuwa maisha yetu yatengenezwa mbali na hali ya hapa duniani. Tutakuwa pamoja na Kristo tukimwona Mungu.
Katika kueleza imani hiyo lazima kuepa mambo yote mawili: tusitoe habari za kitoto (kama malaika wadogo wenye mabawa) wala tusiibomoe imani kwa maneno yasiyoeleweka.


Post a Comment