Ads (728x90)

Powered by Blogger.




Image result for MAISHA MAGUMU
Halmshauri ya manispaa ya Songea mkoani Ruvuma imeendelea kupokea fedha kwa ajili ya mpango wa kunusuru kaya masikini  kupitia mradi wa TASAF awamu ya tatu lengo likiwa ni kupunguza umaskini kwa watu wasiojiweza.
Ofisa habari wa manispaa ya Songea Albano Midelo alisema hadi kufikia  mwezi Mei mwaka 2016 zaidi ya shilingi bilioni moja na milioni 628 zilikuwa zimepokelewa ingawa mwezi Mei,2016 haikupolewa fedha yoyote kwa ajili ya kaya masikini.
Takwimu za mapokezi ya fedha za TASAF awamu ya tatu kwa ajili ya utekelezaji wa mpango wa kunusuru kaya masikini zinaonesha kuwa kuanzia Julai 2015 hadi Mei 2016 zaidi ya shilingi  bilioni 1.628 zilipokelewa na zimeendelea kutolewa kwa kaya masikini za wakazi wa mitaa 95 ya manispaa ya Songea.
 Awamu ya tatu ya TASAF ilizinduliwa rasmi Agosti 2012 Rais mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete ambapo Mpango wa kunusuru Kaya Maskini unatekelezwa ili kujenga uwezo na kuwezesha kaya Maskini kuongeza kipato, fursa na uwezo wa kugharamia mahitaji muhimu na kuboresha maisha.
Kwa mujibu wa Ofisa habari wa manispaa ya Songea,Katika Halmashauri ya Manispaa ya manispaa hiyo uzinduzi wa TASAF awamu ya tatu ulifanyika Januari 5 mwaka 2015 ambapo uzinduzi ulifanywa  na mkuu wa mkoa wa Ruvuma Said Thabit Mwambungu.
Amesema Katika kipindi cha robo ya pili ya mwaka 2015/2016 kazi mbalimbali zimeendelea kufanyika ambazo ni kulipa kaya maskini 7,828 kati ya lengo la kaya 7,915 zilizopo kwenye mpango, ambapo kaya 88 hazikutokea siku ya malipo hivyo fedha zao kurudishwa TASAF Makao makuu kulingana na utaratibu.
Ili kuhakikisha kuwa TASAF awamu ya tatu inafikia ,malengo yake mfuko umetoa mafunzo kwa Watendaji wa Kata, Wauguzi, Walimu wa Shule za Msingi na Sekondari kuwajengea uelewa watumishi hao ili wasaidie katika kuondoa umaskini hasa katika kufuatilia masharti ya elimu na afya.
Mfuko pia umelenga kutoa elimu kwa kaya maskini (wananchi) kuhusu kilimo cha mazao mbadala ambayo hayatumii mbolea za viwandani.wananchi hao masikini walifundishwa kilimo cha mazao ya maharagwe, karanga, alizeti,ndizi, mtama.
Wananchi hao masikini walifundishwa kuandaa mbolea ya asili. Mafunzo haya yalifanyika mwaka 2015 katika mitaa ya manispaa ya Songea ikiwemo Mitaa ya Lilambo A, Mwanamonga na Sinai kata ya Lilambo, Mitendewawa,Chandarua na Muhumbezi kata ya Mshangano,Mletele,Nonganonga na Mdundiko kata ya Mletele, Tanga na Mlete kata ya Tanga,Ndilimalitembo, Mahilo na Chemchem.
Hata hivyo Timu ya ufuatiliaji ya Wilaya na Mkoa ilifanya ziara kwenye mitaa minne  ya Mwengemshindo,Luhira kati, Mitendewawa na Chandarua ili kusikiliza kero za wanufaika wa kaya masikini na kuzitatua.
Uchunguzi umebaini kuwa mpango wa TASAF wa kuzinusuru kaya masikini  umeleta mafanikio ikiwemo kuimarika kwa mahudhurio ya watoto shule za Msingi na Sekondari, kuongezeka kwa mahudhurio ya watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano kliniki na wanufaika wengi kuanza kujiunga na Mfuko wa Afya wa Jamii.
Baadhi ya wakazi wa manispaa ya Songea wameipongeza Serikali kwa kuanza mpango huo wa TASAF awamu ya tatu ambao  wamesema utaleta manufaa kwa Kaya maskini na kusisitiza tangazo la siku ya malipo liwe linatolewa mapema ili kila mnufaika apate malipo kama inavyostahili, pia kwa Walengwa ambao watathibitika kuwa na matatizo kwa siku za malipo, uandaliwe utaratibu maalum wa kuwalipa.
Katika hatua nyingine Taarifa ya idara ya fedha ya manispaa ya Songea inaonesha kuwa  matumizi ya fedha za maendeleo kuanzia Julai 2015 hadi Mei 2016  yalikuwa ni zaidi ya shilingi  bilioni nne na milioni 179.
Mchanganuo wa fedha hizo unaonesha kuwa zaidi ya shilingi milioni 33 zilitumika kwa ajili ya mipango,mfuko wa barabara zaidi ya shilingi milioni 560 na Benki ya Dunia zaidi ya shilingi bilioni moja na milioni 581.
Matumizi mengine ni maji zaidi ya shilingi milioni 72,mfuko wa jimbo  zaidi ya shilingi milioni nne,mfuko wa afya zaidi ya shilingi milioni 102,SEDP zaidi ya shilingi milioni 186 na mfuko wa TASAF awamu ya tatu zaidi ya shilingi bilioni moja na milioni 638.
Halmashauri  ya manispaa ya Songea katika mwaka wa fedha wa 2015/2016 iliidhinishiwa na Bunge kukusanya na kutumia zaidi ya shilingi bilioni 44 na milioni 937 kuanzia Julai 2015 hadi Mei 2016 ambapo mapato halisi  yalikuwa ni zaidi ya shilingi bilioni 33 na milioni 152 sawa na asilimia 73 ya makisio kwa mwaka.
Mwisho


Post a Comment